Na Mwandishi Maalumu, Arusha
WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba amemuelekeza Msajili wa Hazina kufanya tathmini ya utendaji na ufanisi wa Taasisi na Mashirika ya Umma ili aje na ushauri mzuri kwa Serikali ikiwemo kupendekeza kufutwa na kuunganishwa kwa baadhi ya taasisi au kuanzishwa kwa taasisi mpya kama kutakuwa na ulazima huo. 


“Hii itasaidia serikali kubaki na taasisi na mashirika yenye kuleta tija badala ya kuwa mzigo kwa serikali,” ameeleza.


Aidha, amesema hatakubali kuona taasisi, mashirika ya umma na wakala za serikali zinashindwa kuwasilisha hesabu zake kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) mwaka huu, huku akianisha maeneo 10 ambayo wanatakiwa kuyawekea msisitizo na kuimarisha mifumo ya utendaji na uwajibikaji wa taasisi ili zitoe huduma sahihi na endelevu.


Dk Mwigulu aliyasema hayo jana jijini hapa wakati akifungua mafunzo ya mikataba ya utendaji kazi ya Ofisi ya Msajili wa Hazina na bodi za taasisi, mashirika ya umma na wakala za serikali yanayofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Arusha (AICC).


Katika hotuba yake iliyosomwa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dk Khatibu Kazungu, Dk Mwigulu alisema serikali imefanya uwekezaji wa takriban Sh trilioni 65 kwenye taasisi na mashirika yapatayo 237 kwa lengo la kutoa huduma mbalimbali za kijamii, kiuchumi na kusaidia katika kuchangia Pato la Taifa. 


“Ni vyema mkafahamu kwamba taasisi na mashirika haya yanatumia kiasi kikubwa cha fedha za umma kwa njia ya mitaji, mishahara na matumizi mengineyo. Kwa misingi hiyo ni matarajio ya Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ni kwamba, taasisi na mashirika haya yatasimamiwa ipasavyo ili yaweze kutoa huduma sahihi na endelevu,” alisema Dk Mwigulu.


Aliongeza kuwa pamoja na jitihada zinachokuliwa na serikali, bado kuna maeneo 10 ambayo ni muhimu kuweka msisitizo wa kuimarisha mifumo ya utendaji kazi na uwajibikaji wa taasisi hizo.


Aliyataja kuwa ni baadhi ya taasisi bado zinachelewa kuwasilisha hesabu za taasisi kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa ajili ya ukaguzi. “Katika mwaka huu wa fedha na miaka ijayo sitapenda kusikia tena taasisi yoyote ya umma kwamba imeshindwa au kuchelewa kuwasilisha hesabu kwa wakati,” alieleza.
 
“Aidha, taarifa hizo (za utekelezaji za robo mwaka na mwaka) zinazowasilishwa kwa Msajili wa Hazina ni lazima zipitiwe na kumilikiwa na uongozi wa taasisi,” alibainisha na kumuagiza Msajili wa Hazina kuchukua hatua stahiki kwa watakaoshindwa kutekeleza hilo.


Jingine ni kuagiza taasisi na mashirika yote kuhakikisha matumizi yao yanazingatia Mwongozo wa Bajeti wa Mwaka 2021/22 na kanuni zake zinafuatwa ipasavyo katika utekelezaji wa bajeti.


“Na kwa taasisi na mashirika ambayo hazikuzingatia mwongozo wa bajeti hususan kwa fedha za maendeleo, nakuagiza Msajili wa Hazina kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango mzichambue upya na kusitisha miradi yote itakayoshindwa kukidhi matakwa ya mwongozo wa Bajeti kwa mwaka 2021/22,” aliagiza.


Aidha, alisema maombi ya fedha au idhini ya mikopo kwa taasisi na mashirika ya umma yote yapitishwe kwa Msajili wa Hazina kufanyiwa uchambuzi wa maandiko husika kabla ya kuwasilishwa Hazina ili kukidhi matakwa ya Sheria ya Misaada, dhamana na mikopo ya mwaka 1974 kama ilivyorekebishwa 2017. 


Dk Mwigulu alisema hatua hii inalenga kuiwezesha kuwa na kumbukumbu sahihi na udhibiti wa mikopo na matumizi ya fedha kwenye miradi ya maendeleo kwa taasisi na mashirika ya umma.


“Taasisi ziwasilishe michango kwa wakati na kiasi kinachohitajika kwa mujibu wa Sheria ya Msajili wa Hazina na Fedha. Ili kuhakikisha maduhuli na michango inakusanywa ipasavyo na kwa wakati, nakuagize Msajili wa Hazina kuhakikisha makusanyo ya maduhuli ya taasisi zote pamoja na michango yote ya asilimia 15 inakusanywa kwa njia ya kielektroniki,” alibainisha eneo jingine Dk Mwigulu linalopaswa kusimamiwa.


Alisisitiza taasisi kutumia Mfumo wa Mipango na Bajeti (PLANREP), Mfumo wa Kihasibu wa Serikali (MUSE) na Mfumo wa Taarifa za Kimenejimenti na Bodi wa Msajili wa Hazina (OTRMIS) pamoja na mingine yote kama itakavyoelekezwa ili kuimarisha udhibiti wa matumizi ya fedha na utekelezaji wa mipango ya taasisi.


Alisema matumizi ya bodi za wakurugenzi za taasisi yafuate miongozo iliyotolewa na serikali kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina. Aliagiza vitengo vya ukaguzi vya taasisi vidhibiti matumizi ambayo ni kinyume cha miongozo hiyo. 


Pia kwa taasisi za umma ambazo sehemu ya mapato zinakusanya zenyewe, alisema zinapaswa kupunguza utegemezi toka serikali. 


“Bado kuna taasisi nyingi hata matumizi ya kawaida bado zinategemea zilitewe na serikali. Nawakumbusha tena katika hili, zitumieni fursa mlizonazo kuongeza na kukusanya mapato. Kuweni wabunifu kwa kutumia fursa mlizonazo ili kujiongezea mapato. Badilikeni na kuachana na tabia ya kufanya kazi kwa mazoea,” alisema Dk Mwigulu na kuongeza kuwa anatarajia eneo hilo lichangie angalau asilimia 10 ya bajeti za taasisi.


Aidha, aliagiza taasisi ziwe na mipango madhubuti ya kujenga uwezo wa watumishi wa vitengo vya Ukaguzi wa Ndani ili wawe na uelewa mzuri kuhusu majukumu yote ya taasisi pamoja na mifumo mbalimbali inayotumika katika utendaji kazi ili kuviwezesha kuleta tija katika kutekeleza majukumu yake ya ushauri na udhibiti mahala pao pa kazi.


“Mwisho kabisa nikuagize Msajili wa Hazina, nenda kafanye tathmini ya utendaji na ufanisi wa taasisi na mashirika ya umma ili uje na ushauri mzuri kwa serikali ikiwemo kupendekeza kufutwa na kuunganishwa kwa baadhi ya taasisi kama au kuanzishwa kwa taasisi mpya kama kutakuwa na ulazima huo. Hii itasaidia serikali kubaki na taasisi na mashirika yenye kuleta tija badala ya kuwa mzigo kwa serikali,” alieleza Dk Mwigulu.


Alisema ni matarajio yake kuwa masuala hayao yatafanyiwa kazi na taasisi zote na kuhakikisha mapungufu hayo hayajirudii katika taasisi, huku akiagiza kuwa kuanzia mwaka 2022/23 matokeo ya tathmini ya mikataba ni vizuri yawekwe wazi ikionesha taasisi itayofanya vizuri zaidi hadi ile itakayofanya vibaya.  


Awali, Msajili wa Hazina, Athumani Mbuttuka alisema mafunzo hayo yanahusisha washiriki 711 kutoka taasisi, mashirika ya umma na wakala za serikali 237 yaliyoko chini ya Ofisi ya Msajili wa Hazina. 


Mbuttuka alisema katika mwaka huu wa fedha (2020/21), ofisi yake imesaini Mikataba ya Utendaji Kazi na taasisi na mashirika ya umma 230 kati ya taasisi na mashirika ya umma 237 sawa na asilimia 97 ya taasisi zote 237 ambazo zimekeleza matakwa ya kisheria ukilinganisha na mikataba 13 iliyosainiwa mwaka 2014/15

Share To:

msumbanews

Post A Comment: