Na. Angela Msimbira TAMISEMI


WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI) Mhe. Ummy Mwalimu amewataka watendaji wa TAMISEMI kuhakikisha wanafanya kazi kwa ushirikano, ubunifu, uzalendo na uadilifu ili kurahisisha  mtendaji kazi.


Akiongea  leo na Menejimenti  ya ofisi hiyo katika hafla fupi ya ukaribisho  Mtumba,  Jijini Dodoma Waziri Ummy amesema kuwa atahakikisha anafanya kazi kwa ushirikiano, umoja na kujituma ili kuhakikisha TAMISEMI inakidhi matarajio ya Rais na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan


“ Baadhi ya watu wanasema TAMISEMI ni ngumu,  mimi nasema TAMISEMI sio ngumu, kama TAMISEMI ni ngumu maana yake mmeshindwa kunisaidia mimi na Manaibu Waziri kutekeleza wajibu wetu, ila tunakubali ni kubwa lakini hakuna kigumu kama kuna utendaji kazi wa pamoja” amesisitiza Waziri Ummy 


Anaendelea kufafanua kuwa kinachohitajika ni  kufanya kazi kwa umakini, utekelezaji wa majukumu kwa wakati, na kuhakikisha tunaendeleza pale alipoachia aliyekuwa Waziri wa Nchi – TAMISEMI Mhe. Selemani Jafo.


Aidha, Waziri Ummy amesema vipaumbele atakavyoanza navyo kuvifanyia kazi ni kupitia hoja zilizoibuliwa kwenye ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) hasa kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizopata hati chafu nane na zenye mashaka 53.


Amesema vingine ni kuimarisha usimamizi wa makusanyo ya ndani na matumizi katika mamlaka hizo, ushirikiano na ubunifu, usimamizi wa matumizi ya fedha za miradi ya maendeleo na urejeshaji wa fedha za mikopo ya asilimia 10 inayotolewa kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.


Kadhalika, amesisitiza kuzitambua changamoto zilizopo sekta ya afya, elimu na miundombinu ili kuzipatia ufumbuzi.


“Mmemsikia Spika(Job Ndugai) hivi Mkurugenzi unakuwaje na amani wakati watoto wanakaa chini, kitu kama madawati  hivi Mkurugenzi anajisikiaje watoto kukaa chini, hivi sisi TAMISEMI tunashindwa kuja na mkakati wa kuondoa tatizo la watoto kukaa chini, hivi TAMISEMI tunashindwa kuhakikisha madarasa yanajengwa ili watoto wasirundike kwenye madarasa wa kuwa na madawati na madarasa, nyumba za walimu hiki ni kipaumbele changu,”amesema. Waziri Ummy


Kuhusu utoaji wa asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, Waziri Ummy ametaka kujua fedha zilizorejeshwa na kuzitaka Halmashauri kueleza mrejesho ili fedha zitolewe zaidi.


“Sitaki kusema mimi ni hodari bali ni hodari wa kushirikiana na wenzangu naamini tutakwenda vizuri,na kubwa lazima tuonyeshe matokeo hasa kwenye ukusanyaji wa mapato,”amesema.


Aidha amewaagiza Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini(TARURA), kushughulikia hoja zilizobainishwa na wabunge huku akisisitiza suala la uhifadhi na utunzaji wa mazingira.

Share To:

msumbanews

Post A Comment: