Na John Walter-Babati
Iwapo wewe ni miongoni mwa watu ambao hulipa kodi ya zuio kwa ajili ya kupanga nyumba au jengo la biashara, Serikali imesema mwenye nyumba anatakiwa kukurejeshea kiasi cha fedha ulizolipa na si vinginevyo.
Hayo yamebainishwa Bungeni jijini Dodoma baada ya Mbunge wa jimbo la Babati mjini, Paulina Gekul, alipoihoji serikali kuwa ni  lini  itabadili utaratibu wa kumtoza mpangaji wa nyumba ya biashara kodi ya zuio ya asilimia 10 badala ya mpangishaji?
Akijibu swali la mbunge huyo,  Waziri wa fedha na Mipango Dr. Philip Mpango alisema “Kwa mujibu wa Sheria ya Kodi ya Mapato, mpangaji ambaye sio mfanyabiashara na hajasajiliwa na TRA kama mlipakodi hapaswi kukusanya kodi hii”.
Kwa mujibu sheria za kodi nchini Tanzania mpangaji wa nyumba ya biashara husajiliwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na kuwa wakala wa ukusanyaji wa Kodi ya Zuio (Withholding Tax) hivyo kuwa sehemu ya mlipaji wa kodi ya pango.
Sheria ya Kodi ya Mapato inamtaka mmiliki wa nyumba ya biashara mwenye mapato yanayozidi Sh500,000 kulipa kodi ya zuio kutokana na mapato yanayotokana na upangishaji wa pango (rental tax) kwa kiwango cha asilimia 10 ya mapato ya kodi ya pango husika.
Hata hivyo baadhi ya wapangaji ambao hulipa kodi hiyo huwa hawarudishiwi fedha hizo ambazo walitakiwa kukatwa wapangishaji ikiwemo hata kufidiana kwenye kodi.
Dk. Mpango ameliambia Bunge kuwa kodi hiyo ya zuio siyo ya mpangaji, na kwa kuwa Sheria ya Kodi ya Mapato inamtambua mpangaji kama wakala, kiasi cha kodi ya pango ambacho kimelipwa na mpangaji huhesabiwa kama sehemu ya fedha ambazo anapaswa kurejeshewa na mwenye nyumba.
Dk. Mpango amesema kuwa utaratibu wa ukusanyaji Kodi ya Zuio kupitia wakala ambaye ni mpangaji umewekwa ili kurahisisha ukusanyaji wa kodi hiyo, hususan pale mpangishaji anapokuwa hajasajiliwa na TRA kama mlipa kodi.


Share To:

Post A Comment: