Na Mwandishi Wetu
Tanzania imetajwa kuwa nchi ya kwanza Afrika Mashariki na ya nne Afrika kwa kuweka mazingira wezeshi ya ufanyaji biashara ndogondogo.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo Jijini Dodoma, Msemaji mkuu wa Serikali  na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Dkt. Hassan Abbasi amesema kuwa kidunia Tanzania imeendelea kufanya vizuri katika Nyanja mbalimbali ambapo katika suala hilo anasema kidunia imekuwa ya 21.

“Taasisi za Kimataifa zinatambua juhudi za Serikali yetu katika kuwaletea wananchi maendeleo, Baadhi ya masuala yaliyofanyika  kwa wajasiriamali wadogo ni  kupewa vitambulisho maalum vya kuwatambulisha, tozo mbalimbali zimefutwa ili kuwesesha ukuaji wa  sekta ya biashara hapa nchini”,Alisistiza Dkt. Abbasi

Akifafanua  Dkt. Abbasi amesema kuwa Kituo cha Kimataifa cha Televisheni cha CNBC Africa kimerusha makala maalum inayoonesha mafanikio ya Serikali katika kuwaletea wananchi maendeleo na kuoneshwa na zaidi ya nchi 100 Duniani.

Katika makala hiyo iliyoakisi sekta za utalii, miundombinu, nishati, madini, kilimo na uzalishaji, Dkt. Abbasi amesema kuwa hatua hiyo ni moja ya ishara kuwa Taasisi za Kimataifa zinaendelea kutambua hatua zinazochukiliwa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kuwaletea maendeleo wananchi.

Katika hatua nyingine Dkt. Abbasi amesema kuwa Waziri wa  Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki Prof. Palamagamba Kabudi aliwasilisha ripoti ya Tanzania katika Baraza la Dunia la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu  na kusisitiza kuwa Tanzania itaendelea kuheshimu na kulinda haki za binadamu kama ilivyokawaida yake.

“ Haki za Binadamu sio siasa, kama nchi tumeendelea kusisitiza na tutaendelea kuzienzi haki zote za Binadamu kwa maslahi ya watu wote” , alisisitiza Dkt. Abbasi

Tanzania imetajwa kwa nyakati tofauti na Taasisi mbalimbali za Kimataifa kuwa Taifa la kupigiwa mfano kwa namna inavyochukua hatua za kuwaletea wananchi maendeleo, kupiga vita rushwa, kujenga uchumi na ustawi wa wananchi.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: