Na Tito Mselem Dodoma,

Waziri wa Madini Doto Biteko amewakumbusha Viongozi wa Kampuni ya TANCOAL kuanza kulipa deni lao la kiasi cha Dola za Kimarekani 10,408,798 ambalo Kampuni hiyo inadaiwa na Serikali kwa kipindi cha Septemba 2011 hadi Septemba 2019.

Kauli huyo ameitoa leo Novemba 15, 2019 wakati alipokutana na Viongozi wa Kampuni ya TANCOAL inayojishughulisha na uzalishaji wa Makaa ya Mawe katika Mgodi wa Ngaka Mkoani Ruvuma.

Kikao hicho kimefanyika katika Ofisi za Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) Jijini Dodoma na kuhudhuriwa pia na baadhi ya Viongozi Waandamizi wa Wizara wakiwemo Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Augustine Ollal, Mkurugenzi wa Huduma za Sheria Edwin Igenge, Mjiolojia wa Wizara ya Madini Neema Msinde na Mjiolojia Kutoka Tume ya Madini Ezekiel Seni.

Aidha, Waziri Biteko ameisisitiza Kampuni hiyo kuzingatia suala la ushirikishwaji wa Nchi na Wananchi (Local Content), katika shughuli zao na kutoa mfano wa Kampuni ya Shanta Gold Mine kuwa ina asilimia 100 ya Watanzania ambao wanafanya kazi katika mgodi huo ukiwemo Mgodi wa Geita Gold Mine ambao una asilimia 97 za Watanzania ambao wanafanya kazi katika mgodi huo.

Hata hivyo, Waziri Biteko amewakaribisha wawekazaji hao na kuwaeleza kuwa Serikali inataka wawekezaji wake wapate faida na walipe kodi kwa Serikali.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kampuni ya TANCOAL Graeme Robertson ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa hatua inazozichukuwa za kukuza sekta ya Viwanda ambavyo kwa asilimia kubwa huwa zinatumia Nishati ya Makaa ya Mawe katika shughuli za uzalishaji.

Nao, Viongozi wa Kampuni ya TANCOAL wamemshukuru Waziri Biteko kwa maelekezo na ushauri suala ambalo wanaamini itawasaidia katika kupeleka mbele maendeleo la Kampuni hiyo.

Pia, ameongeza kwamba mahusiano mazuri na Serikali ndilo jambo la msingi linaloweza kusaidia katika kukuza uchumi Nchini na Duniani kote, sababu ambayo ilipelekea kukutana na Waziri wa Madini ili kuzunguza masula yatakayo saidia kuboresha uzalishaji wa Makaa ya Mawe katika kampuni hiyo.

Robertson amesema kuwa Kampuni ya TANCOAL ina masoko ndani na nje nchi, ambapo wanunuzi wakubwa wa Makaa ya Mawe nchini ni makampuni ya Saruji, Vigae na viwanda mbalimbali, pia Kampuni husika inasafirisha Makaa ya Mawe kwenda nchi jirani za Kenya, Uganda, Rwanda na Malawi.

“Inchi ya Indonesia inapata pato kubwa kutokana na usafirishaji wa Makaa ya Mawe hivyo naamini hata Tanzania inaweza ikapandisha mapato yake kupitia usafirishaji wa Makaa ya Mawe,” amesema Robertson.

Ameongeza kuwa nchi ya Malawi pia ina kiwango kikubwa cha Makaa ya Mawe isipokuwa tatizo lipo kwenye uchimbaji wake ambapo ni vigumu sana kuyachimba kutokana na mazingira magumu yalipo Makaa hayo ukilinganisha na Makaa yaliyopo Tanzania.



Pia, Robertson amesema Kampuni hiyo inampango wa kuvitumia Vyuo Vikuu vya Tanzania ili kuhakikisha wafanyakazi wa kampuni hiyo wanakuwa na ujuzi wa kutosha katika suala la uzalisha na usafishaji wa Makaa ya Mawe.





Share To:

msumbanews

Post A Comment: