Na.Faustine  Gimu Galafoni,Dodoma.
Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa nchini [TAKUKURU]  mkoa wa Dodoma inamshikilia  Bw.David Daud Tengeneza mwenye umri wa  miaka 50 ambaye ni afisa mtendaji katika kijiji cha Mapanga kata ya Itiso wilaya ya Chamwino  kwa kosa la kushawishi na kujaribu kupokea rushwa   kinyume na kifungu cha sheria Na.15[1]a cha sheria ya kuzuia na kupambana na Rushwa  Sura ya 329 marejeo ya mwaka 2018.
 
Akizungumza na Waandishi wa Habari Ofisini Kwake jijini Dodoma  Nov.5,2019,Mkuu wa TAKUKURU mkoani hapa Bw.Sosthenes Kibwengo amesemaTAKUKURU imekuwa ikipokea tuhuma kadhaa juu ya afisa mtendaji huyo kujihusisha na vitendo vya rushwa .
 
“Mtendaji huyu amekuwa na tuhuma mbalimbali za rushwa ambapo TAKUKURU Mkoa wa Dodoma imekuwa ikifuatilia kwa kina na safari hii arobaini yake imewadia”amesema.
 
Bw.Kibwengo amefafanua kuwa “,baada ya kupokea taarifa mbili tofauti dhidi ya mtuhumiwa  wiki iliyopita tuliamua kufuatilia  mojawapo ambapo uchunguzi ulithibitisha kwamba ameomba rushwa ya shilingi laki tatu[300,000/=]kutoka kwa mtoa taarifa wetu ambaye ni mfugaji.
 
Tarehe 30 Oktoba ,2019 afisa wetu aliambatana na mtoa taarifa  hadi ofisini kwamtuhumiwa ambapo alielekeza apelekewe fedha hizo ndipo ampatie barua  ya kumruhusu  kuingiza kijijini Mapanga  ng’ombe arobaini na nane[48] aliowatoa kijiji jirani cha Segala  la sivyo angemchukulia hatua za kisheria  kwa kutokuwa na kibali.”
 
Mkuu huyo wa TAKUKURU ameendelea kusema kuwa,kutokana na uzoefu wa Mtuhumiwa katika vitendo vya rushwa ,mtuhumiwa alipomwona mtoa taarifa akiwa na mtu mwingine alianza kumhoji huku akisisitiza kuwa yeye ni mzoefu  na mara kadhaa amekoswa na TAKUKURU,hivyo kumtaka akaweke fedha hizo nje ya chooni lakini hakuacha fedha hiyo ya Rushwa na walipoondoka ,mtuhumiwa akaenda chooni kuangalia  na akagundua kuwa hongo yake haipo.
 
Mtuhumiwa aliamua kumfuata mtoa taarifa na kumtaka arudi na akahojiiweje hongo haipo  naye akamweleza hawezi kuacha fedha  bila kupewa barua,ndipo akaelekezwa aiweke chini ya jiwe  lililo chini ya mti  nje ya Ofisi ya mtuhumiwa na aingie ndani kuandikiwa barua.
 
Bw.Kibwengo ameendelea kusema,baada ya kuweka fedha hiyo chini ya jiwe,mtoa taarifa  aliingia ndani ya ofisi lakini mtuhumiwa hakumwandikia barua kwa kisingizio  cha kuisahau mihuri nyumbani na TAKUKURU imemkamata na atafikishwa mahakamani.
 
Hivyo ,Bw.Kibwengo amewakumbusha wananchi wote kuwa ni kosa la jinai kushawishi  na kujaribu kuchukua rushwa  na wananchi wanapokutana na hali hizo watoe taarifa mapema kwa TAKUKURU.
 


Pia,Bw.Kibwengo amewakumbusha watumishi wa Umma kwamba mkono wa sheria ni Mrefu  hivyo ukijihusisha na uhalifu ipo siku ya arobaini itafika na fedheha itakuja ni vyema kuzingatia Maadili ya kazi kwani Rushwa hailipi.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: