Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji (CGF) Thobias Andengenye akizungumza na Mkuu wa Mkoa wa Sogwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela (hayupo pichani).
Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji (CGF) Thobias Andengenye akisalimiana na Mkuu wa Mkoa wa Sogwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela mapema leo wakati wa ziara yake Mkoa wa Songwe.
Mkuu wa Mkoa wa Sogwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela akimsikiliza Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji (CGF) Thobias Andengenye (aliyesimama) mapema leo ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Songwe.

…………………..

Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji (CGF) Thobias Andengenye ameahidi kutoa ushirikiano katika kutekeleza agizo la Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli la kutoa ajira kwa vijana wazalendo waliopanda Mlima Kilimanjaro.

Andengenye ametoa ahadi hiyo mapema leo kwa Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela alipofika ofisini kwake ikiwa ni sehemu ya ziara yake Mkoani Songwe kukagua utendaji wa jeshi hilo Mkoani hapa.

“Suala la ajira za vijana wazalendo waliopanda Mlima Kilimanjaro ili kumuenzi Baba wa Taifa Hayati JK Nyerere kwa sasa linashughulikiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu na watakaponiletea majina niko tayari kutoa ushirikiano.”, amesema Andengenye.

Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela amesema wakati wa kilele cha Mbio za Mwenge wa uhuru kilichofanyika Mkoani Lindi Oktoba 14, 2019 Mhe Rais aliagiza Vijana wazalendo ambao walipanda mlima Kilimanjaro na hawana ajira waangalie namna ya kuajiriwa.

“Tutashukuru sana endapo vijana wetu hawa wazalendo watafanikiwa kupata Ajira, Nchi nzima walipanda vijana 84 kwetu Songwe tulitoa vijana 21 kati yao vijana ambao hawana ajira ni vijana sita kutoka Songwe.”, amesema Brig. Jen. Mwangela.

Wakati huo huo Andengenye amesema kuna mikakati ya kitaifa ya kuboresha utendaji wa jeshi la Zimamoto na Uokoaji na katika Mikakati hiyo Mikoa mipya kama Songwe itapewa kipaumbele hasa katika kuongezewa vifaa na watendaji.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: