Dk Avemaria Semakafu ambaye ni Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia amewataka wanaoibeza elimu ya Tanzania kuacha tabia hiyo kwani ni kujidhalilisha.

Dk Semakafu alisema hayo jijini Dodoma katika hafla ya kuwatunuku vyeti na zawadi washindi wa kikanda na kitaifa wa mashindano ya uandishi wa insha kwa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) na wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

Alisema baadhi ya Watanzania wamekuwa wakiibeza elimu ya Tanzania na kuithamini elimu ya nchi jirani, jambo ambalo si jema kwa kuwa elimu ya Tanzania iko vizuri.

"Hawa watoto walioshinda wamesoma hapa Tanzania na wameenda kuiwakilisha nchi katika mashindano hayo na wamewashinda wao ambao ndio wanaoonekana elimu yao ipo bora kuliko Tanzania, tukiendelea kuidhalilisha elimu yetu ni kujidhalilisha," alisema Dk Semakafu.

Alisema tukio la kuwatunuku washindi hao linatuma ujumbe kwa wale ambao kila uchwao wanaisema vibaya elimu ya Tanzania na kuziponda shule za serikali na kusisitiza kuwa kipimo cha utu ni mtu mwenyewe.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: