WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema hakuna michango yoyote itakayokusanywa kutoka kwa wazazi kwa ajili ya shule kama haina kibali cha Mkurugenzi wa Halmashuri.

“Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. John Pombe Magufuli alishapiga marufuku michango ya aina hii na akatangaza mpango wa elimumsingi bila malipo. Sasa hivi zinaletwa zaidi ya sh. bilioni 20 kila mwezi kwa ajii ya kuboresha elimu ya msingi katika kila wilaya.”

Waziri Mkuu ametoa katazo hilo jana (Jumapili, Julai 15, 2018) wakati akizungumza na maelfu ya wananchi waliohudhuria mkutano wa hadhara kwenye uwanja wa Taifa wa Kahama, wilayani Kahama mkoani Shinyanga.

Alikuwa akijibu hoja ya Mbunge wa Kahama, Bw. Jumanne Kishimba ambaye alisema kuna michango inatozwa bila kibali chochote na kwamba kila kaya inatakiwa ilipe sh. 20,000. “Michango hii itolewe kwa kibali ina iangalie uwezo wa familia kiuchumi,” alisema.

Akitoa mfano, Mbunge hiyo alisema kuna familia ina madebe matatu tu ya mahindi ukiitoza hiyo hela, manake wauze mahindi yao yote ndiyo walete  michango  hiyo wabaki na njaa kwa mwaka mzima. Ni vema michango hiyo izingatie kipato halisi cha kaya,” alisema,

Katika hatua nyingine,Waziri Mkuu aliwaeleza wananchi hao juhudi mbalimbali ambazo Serikali imezichukua ili kuboresha maisha ya Watanzania kupitia huduma za maji, umeme, elimu na afya.

Alisema ameridhishwa na ujenzi wa viwanda unaoendelea kwenye mkoa wa Shinyanga na kukiri kuwa ameguswa kuona kuna uzalishaji mkubwa wa mafuta ya kula yanayotokana na mazao ya mbegu kama pamba na alizeti wakati kuna watu wanaagiza mafuta ya kula kutoka nje ya nchi.

“Nimetembelea kiwanda cha kukamua mafuta ya pamba cha Kahama Oil Mills, na mwenye kiwanda ameniambia kuwa miaka yote huwa anafanya kazi kwa miezi mitatu tu lakini mwaka huu ana uhakika wa kufanya kazi kwa miezi tisa, kutokana na jinsi ambavyo wakulima wameitikia wito wa kufufua zao la pamba,” alisema.

“Jana pia nilitembelea kiwanda cha JIELONG ambacho kiko kwenye Manispaa ya Shinyanga. Na kwenyewe nimeona uzalishaji mkubwa wa mafuta ya kula ambao sijapata kuona,” alisema Waziri Mkuu.

Mapema,Waziri Mkuu alizindua kituo cha afya cha Mwendakulima ambacho kilianza kujengwa mwaka 2010 na kukamilika mwaka 2016 kwa ufadhili wa kampuni ya kuchimba madini ya ACACIA kupitia mpango wake wa Corporate Social Responsibility.

Kampuni hiyo imejenga chumba cha wagonjwa wa nje (OPD), nyumba mbili za watumishi (2 in 1) ambazo zinakaliwa na watumishi wanne, wameweka vitanda na solar panel kwa gharama za dola za Marekani 710,000/- (kwa exchange rate ya kipindi hicho).
Share To:

msumbanews

Post A Comment: