Watu watatu wakiwemo polisi jamii wa Mbezi Luis jijini hapa wamefikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi baada ya kukutwa na meno ya tembo ya thamani ya Sh239.5 milioni.

Wakili wa Serikali Faraja Nguka leo Jumatatu Julai 9, 2018 mbele ya Hakimu Mkazi, Ally Salum amesema washtakiwa hao wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi namba 45 ya 2018.

Amewataka washtakiwa hao kuwa ni Juma Myali (35), Greyson Muhapa (wote polisi jamii) pamoja na Kefas Mlenzi, dereva na mkazi wa Mbezi Luis.

Amesema washtakiwa hao kwa pamoja Juni 28, 2018 katika eneo la Mbezi Wilaya ya Ubungo walikamatwa wakiwa na vipande 30 vya meno ya tembo vyenye thamani ya dola  105,000 za Marekani sawa na Sh 239,505,000, bila kuwa na kibali cha mkurugenzi wa wanyama pori.

Baada ya kusomewa shtaka hilo, hawakuruhusiwa kuzungumza chochote kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kuisikiliza kesi hiyo.

Upande wa mashtaka umedai kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika na hivyo kuahirishwa hadi Julai 23, 2018
Share To:

msumbanews

Post A Comment: