Waziri wa Habari,Utamaduni, Sanaa na Michezo Mheshimiwa Dkt. Harrison Mwakyembe amemwagiza Msajili wa Vyama vya Michezo nchini kuwaandikia barua kali ya onyo Kampuni mbili zinazoendesha Mchezo wa Ngumi za kulipwa nchini.
Mheshimiwa Mwakyembe ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza na vyombo vya habari kwa ajili ya kutoa taarifa ya kazi inayoendelea kufanyika na Kamati aliyoiunda kwa ajili ya kuunda Katiba itakayosimamia Mchezo wa Ngumi nchini ambapo anatarajia kufanya kikao kikubwa cha wadau wake mwezi Juni mwaka huu.
“Nimemwagiza Msajili wa Vyama vya Michezo kutoka Baraza la Michezo la Taifa Tanzania ifikapo kesho kuwaandikia barua kali ya onyo Kampuni mbili zinazoendesha mchezo wa ngumi za kulipwa nchini ambazo ni Tanzania Proffesional Boxing Organization (TPBO) na Pugilistic Syndicate of Tanzania (PST) kutokana na viongozi wake  kuingilia shughuli za Kamati ya kuboresha Katiba ya Ngumi niliyoiunda pamoja na kukashifu na kudharau maagizo ya serikali”,alisema Dkt.Mwakyembe.
Akiendelea kuzungumza katika mkutano huu Mheshimiwa Mwakyembe aliongeza kuwa  kama viongozi wa kampuni hizo za TPBO na PST wataendelea kukashifu na utaratibu unaotumika sasa,amempa Mamlaka Msajili wa Vyama vya Michezo kuwafutia kabisa usajili kwani serikali haitavumilia kuona mchezo wa boxing unaendeshwa bila kuzingatia utaratibu.
Kwa upande wa Mwenyekiti wa Kamati ya kuunda Katiba ya kusimamia mchezo wa ngumi nchini Bw.Emmanuel Salehe alieleza kuwa kazi ya kuandaa Katiba hiyo imekuwa na changamoto nyingi ikiwemo baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo kuleta mvurugano mpaka kufika uamuzi ya kuwapunguza wajumbe sita.
“Kumekuwepo na changamoto nyingi ikiwemo baadhi ya wadau wa mchezo wa ngumi za kulipwa kutoa maneno ya kashfa kwa Kamati pamoja na kudharau utekelezaji wa baadhi ya majukumu waliyopewa kama ya kutoa vibali kwa mabondia wanaokwenda katika mapambano nje ya nchi,”Bw.Salehe.
Pamoja na hayo Waziri huyo mwenye dhamana na Michezo alihitimisha kwa kusema kuanzia sasa ni lazma mabondia wote wanaokwenda nje ya nchi katika mapambano ya ngumi kupata kibali kinachotolewa BMT kwa kuzingatia ushauri unaotolewa na kamati hiyo ya mpito na kwa upande wa uhamiaji atawaeleza hilo ili kuhakikisha mabondia wanaokwenda nje ya nchini wanakwenda kuiwakilisha nchi vizuri na siyo kuuza mchezo.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: