Na Mwandishi Wetu – Mwanza
Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,  Wazee na Watoto Idara ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGOs) imesema haitasita kulifutia usajali Shirika lolote lisilo la Kiserikali litakaloenda kinyume na Sheria na Taratibu za nchi.

Hayo yamesemwa jana Jijini Mwanza na Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Bw. Marcel Katemba alipokuwa akifungua kikao kati yake na Wasajili Wasaidizi wa Mashirka Yasiyo ya Kiserikali na Wadau wa mashirika hayo kwa Mkoa wa Mwanza.

Bw. Katemba amesisitiza kuwa kwa mujibu wa Sheria namba 4 ya Mwaka 2002 ya Mashirika Yasito ya Kiserikali inayataka Mashirika hayo kuzingatia Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo ya Nchi katika utendaji wa kazi zao kwa mujibu wa Katiba na majukumu yao kiusajili.

Ameongeza kuwa kikao hicho kimefanyika ili kuwakumbusha wadau wa NGOs kufanyakazi kwa kuzingatia Sheria za nchi zilizopo kwani baadhi ya mashirika hayo yamekuwa yakitumika kufanya mambo ambayo yapo kinyume na Sheria.

“Nawataka wamiliki wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kuzingatia matakwa ya usajili wao katika kutekeleza majukumu katika Mashirika yao” alisema Bw.Katemba

Bw.Katemba amesema kuwa mpaka sasa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali 4,868 ndio yamehakikiwa na kuyataka Mashirika ambayo hayajahakikiwa  yafanye utaratibu wa kuhakiki kwani mara baada ya kuzinduliwa kwa Tovuti mpya ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini Mashirika ambayo hayatakuwa yamehakikiwa hayataruhusiwa kufanya kazi nchini.

Naye mdau kutoka Shirika la Baraka Orphanage Bi. Patricia Kamugisha asema kuwa kikao hicho imewasaidia kujifunza mambo mengi ambayo walikuwa hawajafahamu na kuendelea kupata uzoefu utakaowasaidiza kuimarisha utendaji wa shughuli katika mashirika yao.

“Sisi kama wadau wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali tunatakiwa kuzingatia Sheria na Taratibu zilizopo ili tuweze kufanya kazi bila kukinzana na Sheria” alisisitiza Bi. Patricia.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: