RAIS
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amewataka
maofisa wa Jeshi la Polisi na Makamishna wake kutoyafyeka na kuyachoma
moto mashamba ya bhangi na badala yake watumie njia za kiintelijensia
kuwababini watuhumiwa, kuwakamata na kuwashughulikia ikiwa ni pamoja na
kuwafikisha katika vyombo vya sheria.
Rais
ameyasema hayo leo wakati akiwahutubia wananchi wa Arusha katika Uwanja
wa Amri Abeid baada ya kuzindua kituo cha polisi na nyumba za polisi
mkoani humo.
“Hakuna
kitu kinachonikera kama Askari Polisi kwenda kufyeka mashamba ya
bhangi, makamanda wako na askari wako, wasikate mashamba ya bangi,
hawakuajiriwa kufyeka bhangi. Niwashauri tu kwamba, tumieni njia za
kintelijensia, mtawashika tu, kama shamba lipo karibu na kijiji, kamata
kijiji kizima, wazee, vijana, wanawake hata na watoto, ndio wakafyeke
hilo shamba la bhangi.
“Nasema
askari wasiende kufyeka bhangi, hawakuajiriwa kufyeka bhangi, usiwatume
askari wako kufyeka bhangi, wataumwa nyoka bure, wamevaa uniform nzuri,
msidhalilishe jeshi kwa kufyeka bhangi, mimi nisingefyeka bhangi na wa
kufyeka wapo.
“Nilimuona
Waziri naye yumo anafyeka na kuchoma moto shamba la bhangi, juzi
nikaona tena RPC wa Dodoma naye anafyeka shamba la bhangi na askari
wake, mpaka akachoka anasema hili shamba lililobaki tutalimalizia kesho.
Inashangaza sana, tusijidhalilishe hivyo,” alisema Magufuli.
Aidha,
Rais Magufuli amelitaka Jeshi la Polisi na vyombo vingine vya Usalama
kuendelea kuimarisha hali ya amani nchini na kuwatumikia Watanzania kwa
maendeleo ya Taifa.
Post A Comment: