Klabu ya soka ya Mtibwa Sugar inayoshiriki ligi kuu soka Tanzania bara imesema haijawahi kulipwa na klabu yoyote ili ifungwe kama ambavyo imekuwa ikidaiwa na baadhi ya mashabiki wa mchezo huo nchini.

Hayo yamebainishwa na kocha mkuu wa timu hiyo Zuberi Katwila wakati akiongea kuelekea mchezo wa leo jioni wa ligi kuu dhidi ya Simba utakaopigwa kwenye uwanja wa Jamhuri Morogoro.

''Nadhani ushindi wetu dhidi ya Azam kwenye robo fainali ya FA na ushindi dhidi ya Singida United sasa umefuta kauli za kwamba tunauza mechi haswa tulipofanya vibaya mwanzoni mwa mzunguko wa pili ambapo kila mtu alisema lake'', amesema.

Katwila ambaye ni mchezaji wa zamani wa timu hiyo ameongeza kuwa leo timu yake itawakosa nyota kadhaa ambao ni walinzi Issa Rashid pamoja na Salum Kanoni ambao ni majeruhi.

Aidha katika mchezo wa leo pia Mtibwa Sugar itakuwa inakosa huduma ya mshambuliaji wao Kevin Sabato ambaye anatumikia adhabu ya kuwa na kadi tatu za njano hivyo kanuni za ligi hazimruhusu kucheza mchezo wa leo.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: