Simba inasubiri pointi 14 tu ili itangaze ubingwa wa Ligi Kuu Bara, sasa kocha wake Pierre Lechantre amesema anachofanya sasa ni kuandaa kikosi bora na cha ushindani kwa msimu ujao.

Lechantre raia wa Ufaransa ameenda mbali kusema anaridhishwa na uwezo wa timu yake msimu huu, lakini kuna marekebisho atayafanya ili msimu ujao watishe zaidi.

Simba leo Jumamosi inacheza mechi ya ligi kuu dhidi ya Lipuli FC kwenye Uwanja wa Samora mjini Iringa na lengo lao ni kushinda ili kuzidi kuiacha Yanga katika msimamo wa ligi hiyo.

Simba sasa inaongoza ligi ikiwa na pointi 58 ikifuatiwa na Yanga yenye pointi 47, hivyo inahitaji pointi 14 ili kujihakikishia ubingwa wa ligi hiyo.

Lechantre alisema kwa sasa anakiandaa kikosi hicho kuwa bora zaidi kwa msimu ujao jambo ambalo linaweza kuwa tishio kwa wapinzani.

“Tunataka kuitengeneza Simba iwe bora zaidi kwa ajili ya msimu ujao, hilo ndilo kusudio letu na si kitu kingine,” alisema Mfaransa huyo aliyechukua mikoba ya Mcameroon, Joseph Omog aliyetimuliwa Desemba, mwaka jana.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: