Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Jenista Mhagama amefunguka na kutoa ushauri kuhusu suala la maandamano na kusema kuwa mtu yoyote ambaye ana ratibu maandamano lazima afuate sheria hata kama maandamano yanatambulika kikatiba.

Jenista Mhagama amesema hayo bungeni na kudai kama kila mtu ataamua kuandamana kwa kuwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaruhusu hilo litakuwa jambo ambalo si sawa hivyo amevitaka vyama vya siasa kufuata sheria za nchi na si kuvunja sheria za nchi.

"Suala la maandamano katika nchi yetu ya Tanzania linaratibiwa na sheria za usalama ndani ya nchi chini ya vyombo vya usalama hasa polisi na Katiba haiwezi kuchukuliwa kwamba ni kigezo cha kuviruhusu vyama kufanya maandamano bila kuzingatia taratibu na sheria zilizowekwa.

"Ninaomba sana Watanzania wote na niviombe vyama vyote vya siasa katika nchi yetu ya Tanzania wahakikishe wanazingatia sheria. 

"Katiba yetu imeruhusu maandamano lakini maandamano yameratibiwa kisheria na kama yameratibiwa kisheria lazima tuhakikishe kwamba tunazingatia sheria katika kuratibu maandamano nchini kwetu Tanzania"

Jenista Mhagama aliendelea kutoa maelezo kuhusu masuala ya maandamano

"Labda niulize swali moja tukiamka hapa siku moja asubuhi na kila mtu ameamua kuandamana wakulima, wafanyakazi yaani kila mtu aamue tu kuandamana kwa sababu tu Katiba imesema nadhani itakuwa siyo sawa na nichukue nafasi hii kuviomba vyama vya siasa kuheshimu Katiba na sheria katika kutekeleza wajibu wao na siyo kuvunja sheria za nchi yetu Tanzania"
Share To:

msumbanews

Post A Comment: