Naibu Waziri wa  Wizara ya  Elimu, Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa William Ole Nasha ameitaka Wizara yake kufanya uchunguzi na kutoa ripoti ya namna ukarabati wa Miundombinu ulivyofanyika katika Chuo cha Ualimu Butimba ili kujiridhisha kama kweli ukarabati huo unaakisi kiasi cha fedha zilizotolewa.
Naibu Waziri Ole Nasha ametoa kauli hiyo Mjini Mwanza baada ya kufanya ziara katika chuo hicho hapo  ambapo amesema hajaridhishwa na ukarabati ulivyofanyika kwa kuwa Chuo hicho kilipatiwa kiasi cha takribani  Milioni Mia Nane Sitini na Tatu.   
Ole Nasha  amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha Vyuo vya Ualimu vinakuwa na mazingira mazuri ya kuwaandaa Walimu wanaokwenda kufundisha katika shule mbalimbali  hapa nchini hivyo ni jukumu la  Wakuu wa Taasisi na Vyuo vya Elimu kuhakikisha wanasimaia Miradi mbalimbali ya Elimu kwa ukamilifu  na kuwa Serikali haitasita kuchua hatua kwa yeyote atakayeshindwa kusimamia Miradi hiyo kwa weledi.
“Chuo hiki kimepatiwa takribani Milioni Mia Nane Sitini na Tatu kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu kama hivi ndivyo ukarabati uliofanyika hauonyeshi thamani ya fedha iliyotolewa kwa ajili ya Chuo hiki cha Ualimu Butimba, kwa kweli Sijaridhishwa”alisisitiza Naibu Waziri huyo.
Akitoa maelezo Mkuu wa Chuo hicho John Ole Meiludie amejitetea kuwa kazi hiyo ya ukarabati imefanyika kwa umakini isipokuwa wanafunzi wenyewe  ndiyo wanachana nyavu za madirisha lakini pia hali ya mvua zinaponyesha huondoa  rangi ambayo  inakuwa imepakwa katika majengo ya Chuo hicho.
Akiwa Mkoani Mwanza Naibu Waziri Ole Nasha ametembelea Shule ya Sekondari Nyegezi iliyoko Wilaya ya Nyamagana na Chuo cha Ufundi Stadi na Huduma VETA kilichopo wilaya ya Ilemela na kuridhishwa na namna walivyotekeleza miradi ya Elimu.

Imetolewa na;
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,
WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA
05/03/2018








Share To:

msumbanews

Post A Comment: