Kamanda Mambosasa
Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es salaam limesema kuwa Mwanafunzi Abdul Nondo ambaye alizua gumzo wiki iliyopita baada ya kupotea katika mazingira ya kutatanisha, hakutekwa bali alifanya hivyo kwa sababu anazozijua mwenyewe.
Akizungumza na Waandishi wa Habari, Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es salaam, Lazaro Mambosasa amesema kuwa upelelezi uliofanyika umeonesha kuwa Abdul Nondo alienda Iringa kwa mpenzi wake na hakutekwa kama watu walivyokuwa wanadhania.
Jeshi la Polisi kanda maalumu ya Dar es salaam kushirikiana na  polisi mkoani Iringa tumefanya uchunguzi na ufuatiliaji na kubaini kuwa mwanafunzi huyo hakutekwa bali alijiteka mwenyewe au kuamua kutoa taarifa hizo kimsingi zilikuwa na maslahi yake binafsi, pengine alizua hilo kwa kutaka kujipatia umaarufu“amesema Mambosasa na kueleza kilichompeleka Iringa kuwa ni mapenzi.
Upelelezi umeendelea kubaini kuwa Mwanafunzi huyo alikwenda Iringa kwa mpenzi wake ambaye alikuwa akifanya naye mawasiliano mara kwa mara akiwa njiani kuelekea Iringa, hii ni baada ya kufanya uchunguzi wa kisayansi na kubaini muda ule aliyosema ametekwa  simu yake imeendelea kuonesha mawasiliano kati yake na yule binti aliyekuwa anamfuata,“amesema Mambosasa.
Kwa upande mwingine Kamanda Mambosasa amesema kuwa Abdul Nondo ataendelea kushikiliwa na upelelezi ukikamilika atafikishwa mahakamani.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: