Meneja wa Mawasiliano wa Mamlaka  ya Serikali Mtandao (e-GA) Bi. Subira Kaswaga,akizungumza na waandishi wa habari leo Agosti 2,2026 kwenye banda la e-GA wakati wa Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nane Nane yanayoendelea katika viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela Nzuguni jijini Dodoma.

..........

MAMLAKA  ya Serikali Mtandao (e-GA) imesema matumizi ya mifumo ya kidijitali yameendelea kuleta mapinduzi katika sekta ya kilimo kwa kurahisisha upatikanaji wa huduma, kuimarisha usimamizi wa shughuli za kilimo na kuongeza uwazi katika utoaji wa huduma kwa wakulima nchini.
Akizungumza leo Agosti 2,2026 katika Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nane Nane yanayoendelea katika viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela Nzuguni jijini Dodoma, Meneja wa Mawasiliano wa e-GA, Bi.Subira Kaswaga, amesema mamlaka hiyo imejielekeza katika kuunganisha taasisi za Serikali kupitia teknolojia ili huduma zinazowagusa wananchi zipatikane kwa haraka, usahihi na ufanisi zaidi.
Amesema moja ya mafanikio makubwa ni kuanzishwa kwa Mfumo wa e-Kilimo kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo, ambao unarahisisha usajili wa wakulima, ukusanyaji wa taarifa muhimu za sekta, usimamizi wa taasisi zilizo chini ya wizara na utoaji wa vibali mbalimbali vinavyohusiana na shughuli za kilimo.

Kaswaga ameeleza kuwa e-GA imeendelea kupanua matumizi ya teknolojia kwa kushirikiana na Tume ya Maendeleo ya Ushirika, ambapo imejenga mfumo unaosaidia kuimarisha usimamizi wa vyama vya ushirika. Kupitia mfumo huo, wakulima wana uwezo wa kufuatilia masoko ya mazao, mwenendo wa mauzo na kupata taarifa muhimu zinazowawezesha kufanya maamuzi sahihi ya kibiashara.

Katika kuimarisha upatikanaji wa pembejeo, amesema e-GA imeungana na Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) kuanzisha Mfumo wa Usimamizi wa Mbolea (Fertilizer Information System – FIS), unaowezesha usajili wa wazalishaji, waagizaji na wasambazaji wa mbolea pamoja na ufuatiliaji wa bei elekezi ili kuhakikisha mbolea inawafikia wakulima kwa wakati na kwa gharama zinazokubalika.

Aidha, amesema e-GA inaendelea kuunganisha mifumo ya taasisi mbalimbali za Serikali, hatua ambayo imepunguza urasimu, kurahisisha ubadilishanaji wa taarifa na kuongeza kasi ya utoaji wa huduma katika sekta mbalimbali za maendeleo.

Hata hivyo amewataka wananchi wanaotembelea Maonesho ya Nane Nane kutembelea banda la e-GA ili kupata elimu kuhusu huduma mbalimbali za Serikali zinazopatikana kidijitali na kujionea namna teknolojia inavyochangia kuimarisha uzalishaji wa kilimo na maendeleo ya uchumi wa Taifa.
Share To:

Alex Sonna

Post A Comment: