Na. Josephine Majura, WF, Nairobi, Kenya.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), amemwakilisha Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), katika Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Maendeleo ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), unaofanyika jijini Nairobi, Kenya, ambapo viongozi wa Afrika wamejadili mikakati ya kuongeza upatikanaji wa mitaji ya maendeleo na kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji barani humo.
Mkutano huo ulifunguliwa rasmi na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Kenya, Prof. Kithure Kindiki, ambapo umewakutanisha viongozi wa serikali, taasisi za fedha za maendeleo, sekta binafsi na wadau mbalimbali kutoka Afrika na maeneo mengine duniani kujadili namna ya kuimarisha uchumi wa Bara la Afrika kupitia uwekezaji na ushirikiano wa kifedha.
Mhe. Munde, alisema kuwa mkutano huo umeonesha dhamira ya nchi za Afrika kuimarisha ushirikiano katika kuhamasisha rasilimali fedha na kuongeza upatikanaji wa mitaji kwa ajili ya kufadhili miradi ya maendeleo, hatua itakayochochea ukuaji wa uchumi, biashara na uwekezaji barani Afrika.
Alifafanua kuwa, ATIDI imeendelea kuimarisha uwezo wake kupitia ushiriki wa taasisi kubwa za fedha za maendeleo duniani, zikiwemo Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) na Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW), ambazo zimeongeza mtaji katika taasisi hiyo, hatua hiyo itaongeza uwezo wa ATIDI kutoa bima dhidi ya vihatarishi vya uwekezaji na kuwezesha utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo katika nchi wanachama, ikiwemo Tanzania.
Wakati wa majadiliano kwenye mkutano huo, viongozi walisema kuwa changamoto ya upatikanaji wa mitaji ya maendeleo bado ni kikwazo kikubwa kwa utekelezaji wa miradi ya kimkakati katika nchi nyingi za Afrika, ambapo walishauri kuimarishwa kwa ushirikiano wa kikanda pamoja na kuzijengea uwezo taasisi za fedha za maendeleo ili ziweze kutoa mitaji yenye masharti nafuu kwa ajili ya kufadhili miradi ya maendeleo.
Washiriki pia walieleza kuwa matumizi ya mbinu bunifu za kifedha, ikiwemo ushirikiano kati ya serikali, benki za maendeleo na taasisi za bima ya vihatarishi vya uwekezaji, yataongeza imani ya wawekezaji, kupunguza gharama za mitaji na kuharakisha utekelezaji wa miradi yenye tija kwa wananchi.
Aidha, mkutano huo ulisisitiza umuhimu wa kuongeza uwekezaji katika sekta za viwanda, nishati, miundombinu, biashara ndogo na za kati (SMEs), pamoja na miradi ya uchumi wa kijani, sekta ambazo zimeendelea kuwa mhimili wa ukuaji wa uchumi shindani na maendeleo endelevu barani Afrika.
Katika hatua nyingine, Mkutano Mkuu ulipitisha Taarifa ya Mwaka na Hesabu Zilizokaguliwa za ATIDI kwa mwaka wa fedha 2025, ambazo zinaonesha kuendelea kuimarika kwa utendaji wa taasisi hiyo katika kupunguza vihatarishi vya uwekezaji na kuvutia mitaji ya maendeleo kwa nchi wanachama.
Ushiriki wa Tanzania katika mkutano huo unaonesha dhamira ya Serikali ya kuendelea kushiriki kikamilifu katika majukwaa ya kikanda yanayolenga kuimarisha biashara, kuvutia uwekezaji, kuongeza upatikanaji wa mitaji ya maendeleo na kutumia kikamilifu fursa zinazotolewa na taasisi za kifedha za Afrika ili kuharakisha ukuaji wa uchumi na kuboresha maisha ya wananchi.
ATIDI hadi sasa ina jumla ya nchi wanachama 24, ikiwemo Tanzania, Kenya, Uganda, Burundi, Ethiopia na jumla ya Taasisi 14 ikiwemo KfW, AfDB, TDB, na nyinginezo.
.jpg)

Post A Comment: