Wkala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kupitia mradi wa RISE imeendelea kuimarisha ushiriki wa wananchi katika shughuli za matengenezo ya barabara kwa kutumia vikundi vya Kijamii vya Matengenezo ya Kawaida ya Barabara (CBRM) hatua inayolenga kuongeza ajira, kukuza uchumi wa wananchi na kuhakikisha barabara zinabaki katika hali nzuri mwaka mzima.
Akizungumza katika mafunzo ya kuwajengea uwezo wataalamu yanayoendelea jijini Arusha, Mtaalamu wa masuala ya kijamii kutoka TARURA Makao Makuu, Bi. Mwanamisi Abdallah amesema mpango huo ni sehemu ya utekelezaji wa takwa la kisheria linaloelekeza asilimia 30 ya bajeti ya kazi za barabara kutengwa kwa ajili ya matengenezo ya kawaida ya barabara.
Amesema TARURA kupitia Mradi wa RISE imeamua kutumia fursa hiyo kuwafikia wananchi moja kwa moja kwa kuunda na kuimarisha vikundi vya kijamii vyenye wanachama kati ya watano hadi ishirini ambavyo vitashiriki katika utekelezaji wa kazi mbalimbali za matengenezo ya barabara.
"Vikundi hivi vitapatiwa mikataba ya kufanya kazi za kusafisha mitaro, kuziba mashimo madogo, kuondoa vikwazo vinavyokatiza njia, kufyeka majani pamoja na shughuli nyingine ambazo hazihitaji matumizi ya mitambo mikubwa. Hii ni fursa kwa wananchi kupata ajira, kuongeza kipato na kushiriki moja kwa moja katika kuboresha miundombinu ya barabara katika maeneo yao", amesema Bi. Mwanamisi.
Kwa upande wake, Mratibu wa Kitaifa wa Programu kutoka Shirika la Kazi Duniani (ILO), Bw. Dampu Ndenzako amesema ushirikiano kati ya ILO na TARURA unalenga kujenga uwezo kwa wataalamu na kuhakikisha vikundi vya kijamii vinatumika kikamilifu katika matengenezo ya barabara huku vikitoa manufaa ya kiuchumi kwa wananchi.
Amesema uzoefu unaonesha kuwa ushiriki wa wananchi katika matengenezo ya barabara hususan maeneo ya vijijini huongeza umiliki wa miundombinu hiyo, huimarisha huduma za usafiri na usafirishaji na kuhakikisha barabara zinapitika katika misimu yote ya mwaka huku wananchi wakinufaika kwa kupata ajira na kuongeza kipato.
Naye, Meneja wa TARURA Wilaya ya Kongwa Mhandisi Peter Johnson, amesema wilaya hiyo imeanza kutekeleza mpango huo katika mwaka wa fedha 2025/26 ambapo imefanikiwa kuunda vikundi 34 vya CBRM, kati ya hivyo vikundi 31 tayari vimeanza kazi huku vingine vikiendelea kukamilisha taratibu za kuingia mikataba.
Afisa Maendeleo ya Jamii Mkuu kutoka Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Bi. Hidaya Abdallah amesema mafunzo hayo yatawawezesha wataalamu wa maendeleo ya jamii kutambua, kuunda, kusajili na kuvijengea uwezo vikundi kwa kuzingatia miongozo na taratibu zilizowekwa huku wananchi wakipata fursa za ajira, kuongeza kipato na kuchangia maendeleo ya miundombinu na uchumi wa jamii kwa ujumla.
Mafunzo hayo ya siku sita yanawakutanisha Wahandisi na Wataalamu wa Mazingira na Jamii kutoka TARURA Makao Makuu, Ofisi za Mikoa na Wilaya pamoja na Wataalamu wa Maendeleo ya Jamii kutoka Ofisi za Wakurugenzi wa Wilaya kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kusimamia utekelezaji wa mpango huo katika mwaka wa fedha 2026/27.










Post A Comment: