Na. Josephine Majura, WF, Dodoma

Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), ameiagiza Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kusimamia na kuhakikisha Benki na Taasisi zote za Fedha nchini zinajiunganisha kwenye Mfumo wa Kushughulikia Malalamiko ya Watumiaji wa Huduma za Fedha kwa kuwa Mfumo huo utasaidia kutatua malalamiko ya wateja wao. 

Dkt. Nchemba ametoa maagizo hayo wakati akizindua Mfumo wa Kushughulikia Malalamiko ya Watumiaji wa Huduma za Fedha (Sema na BoT) na Mazingira ya Majaribio ya Teknolojia ya Fedha (Bank of Tanzania Fintech Regulatory Sandbox), uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Wizara ya Fedha wa Kambarage jijini Dodoma.

Akizungumzia kuhusu Mfumo wa   Sema na BoT, alisema kuwa Mfumo huo utatoa fursa maalum katika kutatua malalamiko ya watumiaji wa huduma za fedha kwa ufanisi na uwazi na utakuwa suluhisho la malalamiko mbalimbali ambayo yamekuwa yakilamikiwa na watumiaji wa huduma za fedha ikiwemo mikopo umiza (kausha damu).

Aliongeza kuwa Mfumo wa Sema na BoT, utaongeza imani ya umma katika kutumia huduma rasmi za fedha na kuboresha uwajibikaji kwa watoa Huduma za Fedha wanaosimamiwa na Benki Kuu ya Tanzania. 

Aidha, Dkt. Mwigulu, aliwataka watoa huduma za fedha kuhakikisha wanatoa elimu ya fedha kwa wateja wao na umma kama inavyoelekezwa katika Kanuni za Benki Kuu za Kumlinda Mtumiaji wa Huduma za Fedha za mwaka 2019.

Dkt. Nchemba akiongelea kuhusu kuanzishwa kwa Mazingira ya Majaribio ya Teknolojia ya Fedha (Bank of Tanzania Fintech Regulatory Sandbox), alisema Serikali imekusudia kuifanya Tanzania kuwa nchi ya mfano miongoni mwa nchi zinazoendelea katika ubunifu wa teknolojia ya masuala ya fedha, kwa kuweka mazingira yanayovutia uwekezaji wa kiteknolojia na kuwajengea uwezo vijana kushiriki katika kukuza uchumi wa kidijitali.

“Kuanzishwa kwa Mazingira ya Majaribio ya Teknolojia ya Fedha kunadhihirisha dhamira ya Mhe.  Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye anatamani kukuza matumizi ya teknolojia katika sekta ya fedha kuelekee kwenye uchumi wa kidijitali”, alisema Dkt. Nchemba.

Aidha,  alizitaka taasisi za fedha kuendelea kutoa elimu kwa wananchi na kuwasisitiza  kujitokeza kwa wingi wakati elimu ya fedha ikitolewa katika maeneo mbalimbali ili kuwa na uelewa mpana wa masuala ya fedha, elimu itakayowasaidia kupunguza kujihusisha na huduma za fedha zenye masharti yasiyo rafiki.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango-Zanzibar,  Dkt. Juma Malik Akil alisema kuwa kwa niaba ya Serikali wataenda kuusimamia Mfumo huo katika utendaji kazi wake ili kupata matokeo yaliyokusudiwa na Serikali.

Naye Gavana na Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Bw. Emmanuel Tutuba, alisema kuwa Mfumo wa Sema na BoT ni rafiki na utamwezesha kila mtumiaji wa huduma za fedha kuufikia na kuutumia wakati wowote, bila kujali mahali au uelewa wa teknolojia
Aliongeza kuwa mfumo huo utawezesha Taasisi za Fedha kubaini na kushughulikia malalamiko ya watumiaji kwa wakati na kuboresha utoaji wa huduma kwa ujumla.
Share To:

Post A Comment: