Timu ya Wataalamu kutoka Wizara  ya Maliasili  na  Utalii  imewasili katika Wilaya Mbarali, Mkoani Mbeya kuratibu zoezi  maalumu  la kuwaondoa tembo kwenye makazi ya watu katika  kata tano za Igava, Mawindi, Miyobweni, Imalilosongwe na Rujewa ambapo zoezi litaanza katika  vijiji vya Kata ya Igava ambavyo  vimeathiriwa zaidi na uvamizi wa tembo.  

Akizungumzia zoezi  hilo , Mwakilishi  wa  Wizara  ya  Maliasili  na  Utalii  Antonia Raphael amesema  zoezi hilo litafanyika kwa  muda wa siku mbili kuanzia tarehe  08 hadi 09 Mei, 2024 ambapo teknolojia  ya  helikopta  itatumika kuwaswaga tembo hifadhini sambamba na kuwafunga  mikanda maalum ya mawasiliano  (GPS satellite Collars) tembo viongozi wa makundi ili kufuatilia mienendo yao.

Vilevile,  Anthonia amesema kuwa zoezi hilo litaongozwa na Mheshimiwa  waziri  wa Maliasili  na Utalii.

Naye, Dkt. Emmanuel  Masenga  ambaye  ni  Mtafiti  Mkuu kutoka Taasisi  ya Utafiti  wa  Wanyamapori  Tanzania  (TAWIRI) amebainisha kuwa maandalizi  ya zoezi hilo  yamekamilika ambapo timu ya wataalamu kutoka Wizara  ya Maliasili  na Utalii  na taasisi  zake za TAWIRI, TANAPA, TAWA  pamoja  na timu kutoka Wilaya ya Mbarali  zipo uwandani kuhakikisha zoezi la kuwaondoa tembo kwenye  makazi  ya watu linaanza kesho kwa ufanisi.

Dkt.Masenga  amesema teknolojia  ya helikopta  imekuwa  na manufaa katika kuwaondoa tembo kwenye makazi ya watu kwa haraka zaidi.

Naye, mwakilishi  wa  Mkuu wa Wilaya  ya  Mbarali, Donald Mwigombe ambaye pia ni Afisa Tarafa ya Rujewa, ametoa wito kwa wananchi kuchukua tahadhari  wakati wa zoezi la kuwaswaga tembo kutoka kwenye makazi ya watu  ambapo amewataka wananchi kutokusogea karibu na tembo, wakati  zoezi linaendelea ili kuepuka madhara yanayoweza kusababishwa na tembo pindi wanaposwagwa kwa helikopta.

Share To:

Post A Comment: