Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama mkoani Arusha limejidhatiti kuimarisha usalama zaidi hususani wakati huu ambao mkoa huo uko kwenye maandalizi kabambe ya kilele cha siku ya wafanyakazi Duniani (Mei mosi) inayofanyika kitaifa mkoani humo Mei 01.2024 kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid, jijini Arusha

Akizungumza na wanahabari muda mfupi baada ya kukamilika kwa kikao kazi cha maandalizi ya sherehe hizo kilichofanyika leo, Jumamosi Aprili 27.2024 kikiongozwa na Mkuu wa mkoa wa Arusha Paul Makonda, Kamanda wa Polisi mkoani humo ACP Justine Masejo amesema katika kuhakikisha usalama unaimarika kabla, wakati na hata baada ya sherehe hizo pamoja na mambo mengine Jeshi hilo limekuwa likifanya doria za miguu na magari kwenye kila kona ya mkoa huo hivyo kutoa wito kwa wakazi na wageni wanaoingia mkoani humo kufanya shughuli zao kwa uhuru, amani na utulivu 

Amesema suala la ulinzi linaanza na mtu mmoja mmoja kisha jamii kwa ujumla hivyo kutoa wito kwa wananchi pale wanapoona viashiria vya uvunjifu wa amani kwa namna yoyote ile kutoa taarifa haraka kwenye maeneo husika ili hatua stahiki zichukuliwe 

Katika hatua nyingine ACP Masejo ametoa wito kwa wakazi wa mkoa wa Arusha na viunga vyake kuchangamkia fursa zitokanazo na uwepo wa sherehe hizo kwenye mkoa huo kwa kuwa nafasi kama hizo hutazamwa kwa mrengo chanya kwenye jicho la kiuchumi.

Share To:

Post A Comment: