Na Zuena Msuya, Morogoro


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti imeridhishwa na Utekelezaji wa Mradi wa njia ya Kusafirisha Umeme katika Reli ya kisasa (SGR).

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, Daniel Sillo ametoa pongezi za kamati wakati wa ziara ya Wajumbe wa Kamati hiyo kwa lengo la kuona na kukagua utekelezaji wa njia ya kusafirisha umeme katika reli ya kisasa (SGR) iliyofanyika tarehe 11 Desemba, 2023 mkoani Morogoro.

Sillo amesema wameridhishwa na utekeleza wa mradi huo baada ya kuona kazi iliyofanyika kwani kamati hiyo imekuwa ikitenga fedha  za kutekeleza miradi mbalimbali nchini ukiwemo mradi huo.

“Tumeona kazi iliyofanyika hapa, awamu ya kwanza kutoka Dar es salaam mpaka hapa Kinguluwira Morogoro imekamilika kwa 100% tunaipongeza Serikali yetu inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa iliyofanyika, Awamu ya pili kutoka Morogoro hadi Makotopora imekamilika kwa 99%, pia tunaipongeza Wizara ya Nishati kazi kubwa ya utekelezaji na usimamizi wa kazi hii, kama Kamati tumeridhika”, amesema Sillo.

Amewahimiza watekelezaji wa Mradi huo kukamilisha kwa wakati  mambo machache yaliobaki ili mradi huo ukamilike kwa maslahi ya kukuza uchumi wa nchi na ulete tija kama ilivyokusudiwa.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga kwa niaba ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko, ameishukuru Kamati hiyo kwa kutenga muda na kukagua mradi huo ambao utachagiza shughuli za kiuchumi kwa Taifa.

Amesema Awamu ya Kwanza ya mradi huo, Serikali ilitoa Bilioni 76 ya kujenga njia ya kusafirisha umeme kutoka Kinyerenzi - Dar es salaam  hadi Kinguluwira-Morogoro

Pia serikali imetenga Bilioni 97 kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa Awamu ya Pili ya mradi huo kutoka Morogoro hadi Dodoma.

Naibu Waziri Kapinga amesema kuwa, hiyo ni dhamira ya dhati ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutoa fedha ya kutekeleza miradi ya kimkakati na kutafuta wawekezaji katika miradi yenye tija kwa nchi.

“Niwahakikishie Watanzania kuwa miradi hii inaendelea kutekelezwa vizuri na fedha ambazo zinatolewa na Serikali zinatumika vizuri ili kuwaletea Watanzania Maendeleo.

Tunamshukuru Rais wetu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake ya dhati ya kutoa fedha za kutekeleza miradi ya kimkakati na kutafuta wawekezaji." Amesema Naibu Waziri Kapinga.

Amesema huo ni mradi muhimu sana katika maslahi ya taifa hivyo  Wizara ya Nishati  imedhamiria kusimamia mradi huo kwa weledi mkubwa ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati na uweze kufanya kazi ili kuwaletea tija watanzania na kwamba tayari Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kumalizia mradi huo. 

Amesema licha ya njia hiyo ya umeme kunufaisha treni ya umeme, pia vituo vilivyojengwa kando ya reli hiyo vitaboresha upatikanaji wa umeme katika maeneo husika.

Share To:

Post A Comment: