Ashrack Miraji (Same)    

Mkuu wa wilaya ya Same Kasilda Mgeni ameagiza Taasisi ya Kuzuia na kupambana na rushwa TAKUKURU wilayani humo  kuchunguza tuhuma za upotevu wa fedha zaidi ya shilingi Milioni ishirini mali ya Jumuia ya watumia maji wa Msindo-Kisiwani zinazo daiwa kuliwa na waliokuwa viongozi wa Jumuia hiyo akiwataka pia viongozi wanaotuhumiwa kujisalimisha ofisini kwake ndani ya siku saba kueleza sababu ya kukaidi kuhudhuria kwenye mkutano huo.


Ametoa maagizo hayo akiwa kwenye ziara yake kusikiliza na kutatua kero na malalamiko ya wananchi na kuelezwa upotevu wa zaidi ya shilingi Milioni 20 zilizotokana na malipo ya wateja zaidi ya 100 wa eneo hilo fedha ambazo hazikuonekana wakati wa makabidhiano baina ya viongozi waliomaliza muda wao na vioongozi wa sasa.


“TAKUKURU mfanye uchunguzi wa huu mradi na jumuiya zake, tujue vitugani vilipashwa kuwepo kwenye makabidhiano na watakao bainika hatua zichukuliwe kwa mujibu wa sheria, tulitakiwa kuongelea masuala ya maendeleo mengine kwamba  mmebuni miradi mnataka kujua ni lini serikali inaleta fedha sio malalamiko haya kwamba serikali imeleta fedha na baadhi ya viongozi kutumia ndivyo sivyo”. Alisema mkuu huyo wa wilaya.


Malalamiko mengine ni baadhi ya viongozi kuwabambikizia kesi wananchi wanao toa taarifa kufichua hujuma zinazofanywa na viongozi hao ambao ni wa serikali na kisiasa ambapo amekemea vikali tabia hiyo na kuagiza jeshi la Polisi kufanya kazi yao kwa kuzingatia taratibu za kisheria pia kuwataka wananchi kupeleka kwa siri majina ya viongozi wenye tabia ya kutoa vitisho.


Aidha mkuu huyo wa wilaya ameagiza Meneja wa RUWASA Wilayani humo kufanya mkutano kwenye eneo hilo kujiridhisha endapo wajumbe waliopo kwenye Jumuiya ya sasa wamekidhi vigezo vinavyo hitajika baada ya kuwepo taarifa ya kuwepo baadhi ya viongozi wa kisiasa waliojiingiza kuwa wajumbe wa bodi ya sasa na kuleta malalamiko.



Mwaka 2021 serikali ya awamu ya sita ilitoa zaidi ya shilingi Milioni 440 zilizotumika kutekeleza mradi wa maji Msindo-Kisiwani na baada ya kukamilika ndipo zikaundwa jumuiya za watumia maji, ikiwemo Jumuiya ya kwanza iliyomaliza muda wake ambayo ndio baadhi ya viongozi wake wanalalamikiwa kuhusika na wizi wa fedha zaidi ya shilingi Milioni 20 ambazo hazikuonekana wakati wa makabidhiano.




 

Share To:

ASHRACK

Post A Comment: