Na. Samwel Mtuwa - Ngara

Imeelezwa kuwa takribani Kaya 1339 katika Wilaya ya Ngara wanatarajia kulipwa kiasi cha zaidi ya Shilingi bilioni 26 ikiwa ni sehemu ya fidia ya ardhi iliyotolewa kupisha mradi wa uchimbaji wa Madini Mkakati ya Nikeli katika eneo la  Bugarama Mkoani Kagera ambapo madini hayo ya Nikeli yatakayochimbwa yatachenjuliwa na kusafishwa hapa hapa nchini Tanzania kupitia kiwanda cha kisasa kitakachojengwa Kahama,Mkoani Shinyanga. 

Hayo yameelezwa leo Novemba 14 , 2023 na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde wakati wa hafla ya Uzinduzi wa Ulipaji  fidia kwa wananchi waliopisha eneo la Mradi wa Uchimbaji wa Madini Mkakati ya Nikeli iliyofanyika katika viwanja vya Mgodi wa Kabanga Nikeli  Mkoani Kagera.

Waziri Mavunde ameeleza kuwa Mradi huu ni wa historia katika nchi zilizo Kusini Mwa Jangwa la Sahara ambao utatumia Teknolojia ya kisasa katika Uchimbaji na Uchenjuaji wa  Madini hayo nchini ambapo teknolojia itakayotumika ni ya kisasa ya hydro met.

Akielezea kuhusu Mipango ya Serikali katika uchimbaji wa Madini  Mkakati , Waziri Mavunde amebainisha  kuwa kwasasa Serikali inaandaa  mkakati wa usimamizi wa madini ya kimkakati na hasa katika kusimamia uongezewaji thamani wa madini hayo hapa hapa nchini. 

Sambamba na hapo Waziri Mavunde amesisitiza kuwa Serikali inachukua Mradi wa Tembo Nikeli kama sehemu ya Mradi wa kielelezo  kwa Miradi mingine ya Madini Mkakati  inayofuata.

Akitoa maelezo yake Waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mh. Jerry Silaa amesema kwamba serikali inatambua umuhimu wa mradi huu mkubwa wa kielezo na kwamba wizara ya ardhi itatoa ushirikiano wa kutosha kuhakikisha kwamba zoezi la fidia linakamilika kwa wakati na wananchi wanapata haki yao kwa mujibu wa Sheria.

Wakitoa maelekezo ya Kamati za Bunge za Ardhi,Maliasili na Utalii na Nishati na Madini,Waheshimiwa Timothy Mnzava na Kirumbe Ng’enda wameitaka Kampuni ya Tembo Nikeli kuhakikisha inalipa fidia kwa wakati kwa wananchi wanaopisha mradi huo wa kimkakati.

Zoezi la uzinduzi wa ulipaji fidia lilishuhudiwa na Mkuu wa Mkoa wa Kagera Hajat Fatma Mwasa,Wajumbe wa Kamati za kuduma za Bunge zinazosimamia sekta za Ardhi na Madini,pamoja na Mbunge wa Ngara Mh. Ndaisaba George na wa viti maalum Mh. Olivia Semguruka.


VISION 2030: MADINI NI MAISHA NA UTAJIRI

Share To:

Post A Comment: