Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Mwanafunzi mwenye umri wa miaka 16 anayesoma kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari Kolandoto iliyopo Manispaa ya Shinyanga, amedai kupewa ujauzito na mzee mwenye umri wa miaka 65.

Mwanafunzi huyo ameileza Redio Faraja kuwa, mzee huyo anayejulikana kwa jina la Amos Samsoni (65) mkazi wa Kijiji cha Mwamala Kata ya Kolandoto, mara ya kwanza alimuita nyumbani kwake na kumpatia kiasi cha Shilingi elfu mbili, ambapo mara ya pili alimuita tena na kumpatia kiasi cha Shilingi elfu tano na kutumia nafasi hiyo kumlazimisha kufanya naye tendo la ndoa.

Waliendelea kuwa katika mahusiano ya kimapenzi tangu mwezi Desemba mwaka jana 2022, mpaka alipobainika kuwa na ujauzito unaokadiriwa kuwa na miezi mitano, baada ya mzee huyo kumtaka kimapenzi ndugu wa mwanafunzi huyo, ambaye alichukizwa na kitendo cha kuwataka wote wawili na kwenda kutoa taarifa kwa kwenye familia.

Taarifa zaidi zinabainisha kuwa, baada ya kikao cha familia kukaa kujadili jambo hilo, walikubaliana mzee huyo atoe faini ya magunia mawili ya mpunga na Baiskeli ili kumaliza suala hilo, ambapo baada ya viongozi wa kijiji kutoa taarifa ya kumwondoa kwenye nafasi aliyokuwa nayo ya Ukatibu kwenye uongozi wa kijiji, kutokana na sababu za kimaadili, wananchi walihoji kutaka kujua kwa undani juu ya hatua hiyo ingawa hata hivyo, hawakupewa majibu ya kuridhisha.

Kufuatia kikao hicho, baadhi ya wananchi ikiwemo wanawake waliamua kufuatilia suala hilo na kubaini kuwa, mzee huyo anatuhumiwa kuwa na tabia za kuwarubuni kimapenzi watoto wadogo ikiwemo mwanafunzi huyo, ambapo walionghea naye na baadaye wakatoa taarifa Polisi.

Kamanda wa jeshi wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kubanisha kuwa, wanaendelea kumtafuta mtuhumiwa huyo kwa kuwa alifanikiwa kutoroka kabla hajakamatwa.

Mganga mfawidhi wa Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Shinyanga Dkt. Luzila John, amethibitisha binti huyo kuwa na ujauzito wa miezi mitano, baada ya kufanyika kwa vipimo vya kitaalam.

Kufuatia tukio hilo, Katibu wa kampeni ya kupinga ukatili ya Waziri Dkt.Dorothy Gwajina (SMAUJATA) Mkoa wa Shinyanga, Bwana Daniel Kapaya,  ameliomba Jeshi la Polisi kuhakikisha mtuhumiwa huyo  anakamatwa na kumfikisha katika vyombo vya sheria.

Share To:

Misalaba

Post A Comment: