Denis Chambi, Tanga.

CHAMA cha ACT Wazalendo jimbo  la Tanga kimesema kuwa changamoto zinazowakumba wafanyabiashara hapa nchini zisimalizwe  kisiasa bali itafutiwe mbinu mbadala wa kuondoa vikwazo  wananvyokabiliana navyo ikiwemo kuundwa kwa tume maalum itakayotoa bei elekezi ili kuondokana na  adha mbalimbali zinazoweza kujitokeza.

Wakisisitiza kauli hiyo kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika   soko la Ngamiani ,vigogo wa chama hicho Thobias Haule  ambaye ni mwenyekiti wa wilaya ya Tanga na mjumbe wa ngazi za juu na  ni diwani wa kata ya Mayomboni wilayani Mkinga Musa Jangwa walisema kuwa zipo changamoto nyingi zinazowakumba wafanyabiashara ambazo zisipopatiwa ufumbuzi wa haraka zinaweza kupelekea mfumuko wa bei ukazidi kuwaumiza wananchi wa hali ya chini .

Mwenyekiti wa chama hicho Thobias Haule alisema kuwa kuna hoja mbalimbali juu ya madhira yanayowakumba wafanyabiashara hapa nchini huku changamoto zikionekana kufanana  zinapaswa  zitatuliwe  haraka ili kurahisisha wananchi kupata bidhaa kwa gharama nafuu na kupunguza mfumuko wa bei za bidhaa  ukiwemo za chakula .

"Changamoto zinajulikana na zipo kwenye mfumo , changamoto za wafanyabiashara zinalingana kila sehemu , wananchi tuamke tudai haki zetu ,tusipo amka kusimamia haki zetu hakuna atakayetusaidia " alisisitiza Haule

Kauli hiyo imekuja kufuatia  mgomo wa wafanyabiashara ulioibuka hivi karibuni jijini Dar es salaam  katika soko la kimataifa la Kariakoo ambapo mara baada ya Waziri mkuu Kassim Majaliwa  kuzungumza na wafanyabiashara hao aliunda tume maalum  itakayopitia changamoto mbalimbali zinazowakabili  ili ziweze kupatiwa ufumbuzi.

Haule alisema bado zipo changamoto mbalimbali zinazowakabili wafanyabiashara hasa wa hali ya chini ikiwemo mazingira duni licha ya kuwajibika kulipa kodi  hali ambayo inayosababisha mzoroto wa kiuchumi huku ubambikizaji wa kesi kwa wananchi ukiwa nao ni kero akiiomba serikali kuzitazama kwa ukaribu.

"Kuna ubambikizaji mkubwa wa kesi hii nayo iangaliwe upya na ifanyiwe kazi haraka , wananchi wanahitaji huduma bora ya maisha ikiwamo bidhaa za vyakula kuwa chini wengi wa wafanyabiashara wakiwemo wamachinga wanafanya shughuli zao katika mazingira magumu na   yanawanyima haki yao wakati huo huo wakiwa wanalipa kodi tunaitaka serikali iwatazame sana wafanyabiashara hawa na kuwawekea mazingira mazuri. " alisisitiza Haule

Aidha alihoji mkoa wa Tanga kufungwa viwanda huku baadhi ya viwanda vikihamisha mitambo kuperekwa nje ya mkoa huo hali ambayo inazidi kuchangia kushuka kiuchumi na kuikosesha serikali mapato.,

"Tanga ilikuwa ni kimbilio la ajira nchini ,kila mmoja alikuwa anakimbilia Tanga kupata ajira katika viwanda mbalimbali  vilivyokuwepo  wakati ule lakini leo hii yamebakia magofu tu ,tunaomba waliopo kwenye madaraka watuambie na watuletee majibu ya maswali ya wakazi wa Tanga kuhusu viwanda" alihoji Haule



 Diwani wa kata ya Mayomboni wilayani Mkinga  Mussa Jangwa akizungumza katika mkutano wa hadhara wa chama hicho uliofanyika soko la Ngamiani jijini Tanga.
Aliyekuwa mgombea wa ubunge kwa tiketi ya chama cha ACT Wazalendo  jimbo la Korogwe mjini mwaka 2020 Bahati Chirwa, akizungumza na wananchama wa chama hicho katika mkutano wa hadhara uliofanyika jijini Tanga May 23, 2023. 




Share To:

Post A Comment: