Mchungaji wa Kanisa la Moravian Tanzania (KMT) Parishi ya Sabasaba Singida, Yona Ezekiel akitoa baraka kwa waumini wa kanisa hilo (hawapo pichani) wakati wa Ibada ya Pasaka iliyofanyika Aprili 9, 2023.

Na Dotto Mwaibale, Singida

KANISA la Moravian Tanzania Parishi ya Sabasaba mkoani Singida limeiomba Serikali kuzifuta Taasisi zote zisizo za Kiserikali (NG'OS) ambazo zinatuhumiwa kuhusika kuhamasisha mapenzi ya jinsia moja (shoga)

Ombi hilo limetolewa na Mchungaji wa kanisa hilo, Yona Ezekiel wakati akihubiri jana katika ibada ya Pasaka ambapo alisema Serikali ichukue hatua za haraka kuyafuta mashirika hayo kwani watanzania hawavitaki vitendo hivyo.

Alisema hivi karibuni aliyekuwa Mbunge wa Kyela na kushika nafasi mbalimbali za uwaziri katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Harison Mwakyembe alisema zipo taasisi nyingi ambazo zimeenea hadi mikoani ambazo zinahamasisha ushoga na wakurugenzi wa taasisi hizo wanajulikana na kuwa walengwa ni vijana.

"Tumeambiwa na Dk. Mwakyembe kuwa taasisi hizi zipo na wahusika nazo wapo tunaiomba Serikali izifute kwani zina waharibu vijana ambao ni nguvu kazi ya taifa na watanzania awahutaki ushoga, usagaji na ukatili wa kijinsia wa aina yoyote kwani na hata vitabu vya dini vimekataza mambo hayo," alisema Mchungaji Yona.

Akihubiri huku akilia na kulifanya kanisa lote kulipuka kwa vilio Mchungaji Ezekiel alisema nchi yetu isikubali kuingia katika vitendo hivyo kwa shinikizo la kupata fedha za mikopo kutoka kwa matajiri ambapo aliwaomba wazazi kuendelea kufuatilia nyendo za watoto wao ambao ndio wa lengwa wa mambo hayo.

Akizungumzia kufufuka kwa Yesu Kristo baada ya kifo chake huku akinukuu kitabu cha Yohana Mtakatifu Sura ya 20 mstari wa kwanza hadi wa nane alisema kufufuka kwake ni ushindi mkubwa kwani Mungu alimleta duniani  ili kuja kuwakomboa wanadamu kutokana na dhambi.

Alisema kifo wakati wote kimekuwa kikiharibu mipango ya watu, kinaleta majonzi, huzuni,mtetemeko  na kuwa hakivumiliki kwani hakichagui mtu na kimekuwa kikiwachukua hata watu waliokuwa wakitegemewa na ndugu na familia zao na ndivyo ilivyokuwa kwa Yesu ambaye kifo chake kilikuwa na fumbo kubwa la imani kwani aliuawa na siku ya tatu alifufuka.

Mchungaji Ezekiel alitumia ibada hiyo ya Pasaka kuwahimiza wakristo kuacha kutenda dhambi na badala yake kuwa na moyo wa huruma wa kusaidia watu mbalimbali wenye uhitaji wakiwepo Yatima, Wajane, wazee, wagonjwa, wafungwa na wengine wote na kuwa kwa kufanya hivyo watabarikiwa na Mungu.

Aidha, Mchungaji Ezekiel amewahimiza wakristo wote wa kanisa hilo kujitokeza kwa wingi kwenye mkutano wa Umoja wa Makanisa mkoani hapa ambao utafanyika Aprili, 10, 2023 Ukumbi wa Kanisa Katoliki (MAARUFU RC) ambao utaanza kwa maandamano yatakayoanzia Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT) Mitunduruni kupitia Barabara ya Kinyeto, TRA, Arusha Road hadi eneo utakapofanyika mkutano huo ambapo Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.

Katika hatua nyingine Mchungaji Ezekiel ameendelea kuwaomba wadau mbalimbali kusaidia ununuzi wa kiwanja cha kujenga Kanisa la Moravian Parish ya Sabasaba kwani hivi sasa wanafanya ibada zao katika kanisa la muda walilolijenga kwa kutumia miti na mabati.

Aliomba kwa mtu yeyote, kiongozi yoyote, Sheikh wa Mkoa wa Singida, Issa Nassoro, Taasisi, Wafanyabiashara na madhehebu mbalimbali watakao kuwa tayari wanaweza kutoa kiasi chochote cha fedha kupitia Akaunti  Namba 50810046663 Benki ya NMB Kanisa la Moravian Sabasaba Singida mjini au awasiliane na Mchungaji Yona Ezekiel kwa namba 0758148508.

Mchungaji, Ezekiel akisisita jambo katika ibada hiyo wakati akiiomba Serikali kuzituta taasisi zote ambazo zimekuwa zikihamasisha ushoga hapa nchini.
Mchungaji Ezekiel akiendelea kusisitiza jambo wakati wa ibada hiyo.
Jemina Kalinga akitangaza matangazo mbalimbali katika ibada hiyo.
Ambwene Obed, akisoma somo la kwanza katika ibada hiyo.
Mtumishi wa Mungu Erasto Lazaro akisoma somo la pili kwenye ibada hiyo.
Mama Mwalwiba akionesha umahiri wa kuimba nyimbo za kumtukuza Mungu kwenye ibada hiyo.

Nyimbo za kumtukuza Mungu zikiimbwa wakati wa ibada hiyo.
Furaha ya kufufuka kwa Yesu Kristo ikitamalaki kwenye ibada hiyo kwa kuimba na kucheza.
Mtumishi wa Mungu Muinjilisti, Abel Mwakajangwa (kushoto) akiongoza kuimba nyimbo za kumtukuza Mungu kwenye ibada hiyo.
Nyimbo za kusifu na kuabudu zikiimbwa.
Vilio vikitawala wakatiMchungaji Yona Ezekiel alipokuwa akiongea kwa uchungu kupinga vitendo vya ushoga hapa nchini.
Ni huzuni na vilio wakati Mchungaji Ezekiel alipokuwa akizungumzia vitendo vya ushoga.
Watoto wa kanisa hilo wakionesha furaha yao katika sikukuu hiyo ya Pasaka.
Wanawake wa kanisa hilo wakiwa katika picha ya pamoja baada ya ibada hiyo ya Pasaka.
 

Share To:

dotto mwaibale

Post A Comment: