Waziri wa nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya utumishi wa umma na utawala bora ,Mhe. Jenista Mhagama amezitaka Taasisi zote za umma nchini kuhakikisha zinazingatia na kufuata sheria, na kanuni za Serikali Mtandao .


Ameyasema hayo Feb 10 jijini Arusha wakati akifunga kikao kazi cha 3 cha Serikali mtandao kilichowashirikisha zaidi ya watumishi wa umma 1600 kutoka mikoa mbalimbali nchini. 


Amesema kuwa,ni lazima taasisi zote za umma zihakikishe zinafuata sheria zilizopo ili kuwezesha kufanya kazi kwa weledi na uzalendo kwa ustawi wa nchi na kuweza kuokoa gharama kupitia huduma za kidigitali. 


“Naagiza mkaanze kufanya vikao vya kitaasisi kila mwaka katika ngazi za wilaya na mkoa katika kuhakikisha mnatathimini huduma ya serikali mtandao katika ngazi za wilaya na mkoa ili huduma hiyo iweze kuboreshwa na kutumia na taasisi zote za umma.”amesema Waziri Jenista .


Aidha amewataka kupitia kikao hicho wakatekeleze maazimio yote waliyojiwekea huku akiwataka kuendana na mabadiliko ya kasi ya duniani ya teknolojia yaliyopo hivi sasa kwani hawatakiwi kuwa nyuma .



“Wataalamu na wakuu wa idara nawaomba sana mhakikishe mnafanya kazi zenu kwa weledi na uzalendo mkubwa kwa faida ya Taifa letu, huku mkihakikisha kila mmoja anakuwa mwaminifu katika usimamizi wa mifumo ya Tehama. “amesema Waziri Mgahama.


Kwa upande wake Mmoja wa washiriki katika mkutano huo,ambaye ni Katibu Tawala wa mkoa wa Njombe ,Judica Omary amesema kuwa,kikao hicho ni cha tatu kufanyika na wameweza kujadili changamoto mbalimbali na kuweka mikakati na maboresho mbalimbali ikiwemo ya kuongeza matumizi ya mtandao serikali. 


Amesema kuwa, kikao hicho kimekuwa na manufaa makubwa kwao watumiaji wa serikali mtandao katika kukuza taaluma zao .


Amesema kuwa,wamejiwekea mikakati ya kuhakikisha wanaenda kutekeleza huduma ya serikali mtandao katika taasisi zao kwa ajili ya kuboresha utendaji kazi wa taasisi zao.


“Kwa pamoja tumejiwekea mikakati ya kuhakikisha tunaenda kufanya vikao vyetu kidigitali katika vikao mbalimbali ikiwemo vikao vya madiwani na kuondokana na matumizi ya makaratasi.”amesema.


Naye Mkurugenzi wa Mamlaka ya serikali mtandao (eGA) ,Mhandisi Benedict Ndomba akielekezea maazimio waliyojiwekea amesema kuwa , kwa pamoja wameweza kujiwekea maazimio mbalimbali ikiwemo kuhakikisha taasisi za umma anatumia huduma ya serikali mtandao katika kuendesha shughuli zake pamoja na vikao vya madiwani ili kuweza kupunguza matumizi ya makaratasi. 


Amesema kuwa,wamejiwekea maazimio ya kuhakikisha tovuti zote zinaboreshwa ili kuweza kwenda kisasa zaidi ,huku wakizitaka taasisi za umma kutoa kipaumbele kwenye maswala ya Tehama .

Aidha amesema kuwa,maazimio mengine ni pamoja na kuhakikisha wakuu wa taasisi za umma kuhakikisha wanasimamia kikamilifu usimamizi wa sheria za serikali mtandao, sambamba na kuiomba serikali kuanzisha upekuzi kwa watumiaji wa huduma za Tehama. 


Kwa upande wake Naibu katibu mkuu ofisi ya Rais,menejimenti ya utumishi wa umma na utawala bora,Xavier Daudi amesema kuwa, wanaenda kuyafanyia kazi mapendekezo yote yaliyotolewa katika kuhakikisha huduma ya serikali mtandao ina imarika zaidi. 


“Tunaendelea kusisitiza zaidi matumizi ya Tehama kwani yatasaidia sana kuokoa gharama ya kutumia matumizi ya makaratasi huku tuhakikisha kunakuwepo kwa matumizi sahihi ya huduma mtandao. “amesema.


Share To:

ELIZA DOM

Post A Comment: