WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema viongozi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wanamatumaini makubwa kuwa mashindano ya shule za msingi na Sekondari za Afrika Mashariki (FEASSSA) yataendelea kuwa chachu kwa nchi washirika kuendelea kuthamini michezo.

 

Amesema kuwa viongozi hao wanaamini kupitia michezo hiyo ya FEASSSA itaendelea kusaidia katika kukuza ajira, kustawisha jamii, uchumi na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa.

 

Amesema hayo leo (Jumapili, Septemba 18, 2022) wakati akizindua Mashindano ya michezo ya shule za msingi na za Sekondari kwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid Jijini Arusha.

 

Mheshimiwa Majaliwa ametumia fursa hiyo kutoa wito kwa Mamlaka zote zinazosimamia elimu katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki kuendelea kuwajengea mazingira rafiki vijana wanaoshiriki michezo ya FEASSSA ili kutanua wigo wa ushindani ndani na nje ya Jumuiya ya Afrika ya Mashariki.

 

“Ni vyema sasa viongozi wa FEASSSA kushirikiana kwa karibu na vyama vya michezo katika nchi za Afrika Mashariki na vilabu vya michezo mbalimbali kutupia macho vipaji vinavyopatikana katika mashindano haya ya wanafunzi ili kupata wachezaji watakaokuwa na mwendelezo na kuvitumikia vilabu vyao.”

 

Aidha, Mheshimiwa Majaliwa amewataka viongozi wa Mashirikisho ya Michezo ya shule katika kila nchi husika kuwa na mipango ya pamoja ya muda mfupi na muda mrefu ya maendeleo ya michezo ya shule. “Mipango hiyo itumike kuhamasisha utekelezaji wa mikakati ya kuendeleza michezo katika taasisi za elimu ndani ya Jumuiya.”

 

 

Amesema ni vyema pia viongozi wa chama hicho kutoa fursa kwa walimu wa michezo wa nchi wanachama kubadilishana uzoefu ili kuboresha ufundishaji wa michezo shuleni.

 

Mheshimiwa Majaliwa amesema michezo hii ya FEASSSA itasaidia kuwafanya wanafunzi kuwa na afya njema ya akili na mwili, hivyo kuboresha ufundishaji na kuendeleza vipaji vya wanamichezo mahiri.

 

“Ni wazi kuwa matatizo mengi ya kiafya kwa wanadamu yanaongezeka kutokana na mfumo mpya wa maisha tunayoishi ambao hautupi muda wa kushiriki shughuli za michezo. Watu wanaoshiriki katika michezo imewasaidia kupunguza matatizo mengi ikiwemo matatizo ya msongo wa mawazo, shinikizo la damu, kisukari na uzito uliopitiliza”.

 

Awali, akizungungumza katika uzinduzi huo Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Mheshimiwa David Silinde amesema, anamshukuru Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake ya dhati ya kuwezesha na kuendeleza michezo hususan katika shule za msingi na sekondari.

 

“Lengo la FEASSSA ni kuimarisha umoja, mshikamano na kuwajengea vijana wetu uzalendo.”

 

Naye, Rais wa Shirikisho la Vyama vya Michezo vya Shule za Sekondari Afrika Mashariki (FEASSSA) Justus Mugisha Amesema moja ya malengo ya Michezo hiyo ni kuhakikisha wanazalisha vijana wataoweza kushiriki katika michezo mbalimbali ili kuzitangaza nchi za Afrika Mashariki.

 

“Tunajua vijana hawa hapo baadae watakuwa sehemu ya timu zetu za Taifa na hatimaye kuitangaza jumuiya yetu, hii ndio maana tunaamini katika michuano ya mashule Ikiwemo hii ya FEASSSA.”

 

Share To:

Post A Comment: