CHUO Kikuu
cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia ufadhili wa Taasisi inayojishughulisha na
tafiti za utunzaji wa Bahari (WIOMSA) wameendesha mafunzo ya Kimataifa ya
kuwajengea uwezo Wanasayansi, Mameneja na wadau wengine namna ya kuendesha na
kufanya tathimini ya Maji kwa Mazingira katika ukanda wa Magharibi mwa Bahari
ya Hindi.
Akifungua
mafunzo hayo jana Septemba 19, 2022 Wilayani Mbarali mkoani Mbeya, Mkuu wa
Wilaya hiyo Reuben Mfune amewataka
wadau waliopata mafunzo hayo kuhakikisha wanakwenda kuyafanyia kazi na
kuwafundisha wengine kwenye ofisi wanazotoka ili kutimiza malengo ya mafunzo
hayo ambayo yanataka kuwepo na utiririkaji wa maji safi na salama kwenye mito
kuelekea baharini mwaka mzima.
“Wale ambao wako ukanda wa juu ya mto
unakoanzia wanatakiwa kujua fika shughuli za uharibifu wanazozifanya kule ndizo
zinazoleta athari kwenye mabwawa ambayo yanajaa tope ambalo linakwenda mpaka
Baharini na kuaathiri viumbe vilivyomo katika Mito, Maziwa na Bahari”, alisema Mfune.
Mfune
amewapongeza SUA na WIOMSA kwa kuandaa mafunzo hayo kwakuwa yanaendana na kazi inayoendelea ya
kurejesha afya ya Mito na kupunguza madhara yanayotokana na uchafuzi wa
Mazingira katika mito, kwani ni jambo jema kufanyika na litakuwa msaada mkubwa
kwa Taifa.
Aidha
alisema zipo shughuli nyingi za kibinadamu zinazofanywa kwenye vyanzo vya maji
na kandokando ya mito kama vile ukataji miti hivyo,ufugaji usionzingatia ukubwa
wa eneo hivyo amewataka Wananchi kuunga mkono jitihada zinazochukuliwa na
serikali katika kusimamia sheria na kanuni zilizowekwa ili kuhifadhi mito na
mazingira kwa faida ya kizazi hiki na kijacho.
“Maji haya
yana umuhimu kwa taifa zima kama bwawa la Nyerere ambalo linajengwa kwa gharama
kubwa. Iwapo litashindwa kufanya kazi kutokana na ukosefu wa maji maana yake
serikali itakuwa imepoteza fedha hizo bure, lakini pia tuna bwawa la umeme la
Mtera na Kidatu haya yote yasipoweza
kufanya kazi tutakuwa tunapunguza uwezo wa kuwa na Tanzania ya viwanda”,
alisema Mfune.
Aidha
amewataka wadau wengine kuendelea kujitokeza kusadia jitihada za Serikali na
wadau waliopo sasa ili kuhakikisha Mito inaendelea kutiririka mwaka mzima na
hivyo kuwataka Wananchi kuheshimu Sheria zilizowekwa kwakuwa zipo kwa manufaa
ya watanzania wote.
Akizungumzia
mafunzo hayo Mtafiti Mkuu wa Mradi huo kutoka (SUA) Prof. Japhet Kashaigili
alisema lengo kubwa la mafunzo hayo ni kujenga Wataalamu na utaalamu wa kuweza
kufanya tathimini ya maji kwa mazingira ili kusaidia wanapofanya maamuzi katika
kugawana maji iwe kwa ajili ya maendeleo endelevu.
“Ni mafunzo
ya kujenga uwezo ambayo yana vitendo ndani yake. wataona shughuLi zinazofanyika
kama sehemu ya kuhifadhi mazingira na kilichopelekea shughuLi hizo zifanyike
pamoja na sababu za msingi za kuwezesha kwanini hiyo tathimini ya maji kwa
mazingira ifanyike na shughuli gani zifanyike kwenye maeneo hayo. Hivyo mahari
kwingine watafanya wao wenyewe kama sehemu ya mazoezi”, alisema Prof.
Kashaigili.
Prof.
Kashaigili amefafanua kuwa tathimini hiyo ya maji kwa mazingira itawezesha
kuhusanisha madhara yanayotokana na shughuli mbalimbali zinazozifanywa na kwa
kiasi gani zinapelekea kuathiri Ukanda
wote wa Bahari ili kuweza kujua chanzo
cha tatizo, hatua tatizo lilipofikia,
madhara na namna ya kutatua.
“Hii
itasaidia nchi kutekeleza Sera ya maji pamoja na Sheria ya maji ya mwaka 2009
ambayo imeainisha katika kugawana maji kwa vipaumbele ni kwa ajili ya matumizi
ya Binadamu, Mazingira na kwa shughuli nyingine, hivyo maji kwaajili ya
mazingira ilikuwa ni sehemu ambayo haina utaalamu na hakukuwa na jinsi ya
kufanya hivyo bila kujenga utaalamu sasa utaalamu upo hivyo ni lazima tujenge
sasa Wataalamu wengi “, alisema Prof. Kashaigili.
Meneja wa Programu ya Mazingira ya Bahari (WIOMSA) ambao ndio wafadhili wa
mafunzo hayo, Dk. Mathias Igulu amesema kuwa kuna mahusiano makubwa kati ya
Bahari na Mito, lakini jambo hilo halijaongelewa sana ndio maana WIOMSA wameona
ni vyema kuanzisha mjadala na kuwaleta pamoja Wanasayansi na wadau wengine kwa maslahi mapana ya uhifadhi wa Bahari,
Mito na Mazingira.
“Kwa
kushirikiana na chuo chetu kikubwa cha SUA ambacho wote tunajua wana Wataalamu
wabobevu kwenye maswala ya Sayansi za Kilimo, Maji na Mazingira, Ufugaji wa
Samaki na Sayansi zingine zinazoendana na hizo tumeona ni muda muafaka
kushirikiana nao kuwaleta pamoja wadau muhimu nchini na nje ya Tanzania kwa
kuwa wanao uwezo mkubwa wa kusimamia” alisema Dk. Igulu.
Ameongeza
kuwa maswala ya Bahari na mito ni mambo yanayogusa maisha ya watu kila siku na
ni swala la kiusalama pia maana jamii inahitaji kutumia maji katika kuzalisha,
hivyo ni jambo muhimu na lazima liangaliwe kwa umakini kwa faida ya nchi zote
zinazoguswa na mambo haya.
Alisema, wataalamu wa mambo hayo ya tathimini ya maji kwa mazingira ni wachache sana
nchini na hii ni kutokana na kutokuwa na chuo kinachotoa Wataalamu mahususi kwa
fani hiyo na hivyo amekiomba Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo kuona umuhimu wa
kuanzisha mitaala ya masuala ya tathimini ya maji kwa mazingira kwakuwa wanao
uwezo na Wataalamu wabobevu.
Akizungumza
mmoja ya washiriki wa mafunzo hayo, Mtafiti Msaidizi kutoka Taasisi ya Utafiti
ya Uvuvi (TAFIRI) Wendo Lukwambe alisema mafunzo hayo yana umuhimu mkubwa
kwao kwakuwa yatawasaidia kujua jinsi mtiririko wa maji unavyoenda na namna ya
kutunza maji kwa mazingira kwakuwa isipofanyika hivyo itasababisha kuathirika
kwa maji hayo.
“Tunajitahidi
sana tujue mawazo na teknolojia za mtiririko wa maji na mazingira kwasababu
zitatusaidia hata katika mambo ya samaki kwenye uvuvi. Kuna baadhi ya samaki
huwa wanapotea kutokana na mazingira jinsi yalivyobadilika ukija kuangalia
chanzo utakuta kinatoka kwenye Maji na Mazingira, hivyo kama tukitunza chanzo
cha Maji vizuri kinaweza kutusaidia hata sisi kwenye Bahari na Samaki pia kwa
kuepusha vifo na kutoweka kwa aina za samaki”, alisema Lukwamba.
Mafunzo hayo ya siku tano yamewahusisha washiriki kutoka Taasisi mbalimbali za Utafiti katika sekta za Maji, Mazingira, Misitu na washiriki wengine kutoka nchi za ukanda wa magharibi mwa Bahari ya Hindi ikiwemo Afrika Kusini, Kenya, Mauritius, Msumbiji, Visiwa vya Shelisheli, Somalia, , Visiwa vya Comoro, Madagasca na Visiwa vya Reunion ambao wameshiriki kwa njia ya Mtandao (Zoom).
Post A Comment: