Na WMJJWM, Dodoma

 

Mwakilishi wa Mkutano wa Dunia wa watoto, Mtoto Victor Paschal Ntatau amemuomba Rais Samia Suluhu Hassan kuhakikisha mazingira Bora ya elimu yanayowapa nafasi ya kujifunza na kuibua vipaji na fursa sawa kwa walemavu na watoto wa Tanzania.

 

Mtoto Victor ametoa wito huo Septemba 19,2022 baada ya kuwasili Jijini Dodoma akitokea nchini Denmark alipowakilisha watoto wa Tanzania kwenye mkutano wa Dunia uliwakutanisha  watoto 60 kutoka sehemu mbalimbali Duniani.

 

"Nimejifunza mambo mengi kwa faida ya watoto na nchi hii. Jumla watoto 60 tuliokusanya mawazo na kutoka na tamko ambalo naamini Rais wangu Mhe. Samia Suluhu Hassan amelisikia" amesema Victor.

 

Katika mkutano huo uliofanyika kati ya tarehe 13-16 Septemba, 2022 watoto wametoa tamko pia kuomba Jamii kuangalia athari ya mabadiliko ya tabia nchi katika ukuaji wa watoto, kwa sababu watoto ni mtaji wa kizazi kijacho.

 

Akipokea Bendera ya Taifa kutoka kwa Victor, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Dorothy Gwajima amesema watoto wana haki ya kushiriki na kushirikishwa kwenye Masuala yanayowahusu.

 

Dkt. Gwajima, amesema mabaraza ya watoto ni msingi wa kuwajenga watoto kupitia klabu shuleni ambazo ndio nguzo za utendaji wa mabaraza ya watoto nchini.

 

"Nikiwa Waziri mwenye dhamana ya watoto, naagiza watendaji wangu kupitia Katibu Mkuu wa Wizara kuhakikisha vipaji vya watoto kama Victor vinatambuliwa na kuendelezwa ili kufikia malengo ya makuzi na utimilifu katika maisha yao ya utoto na hatimaye kuwa raia wenye tija wanapokuwa watu wazima" amesema Mhe. Gwajima 

Share To:

Post A Comment: