Mradi wa ujenzi wa maabara changamano  awamu ya pili  katika Tume ya nguvu za atomu Tanzania ulioanza septemba 16 ,2019 unatarajia kugharimu jumla ya shs 10.4  bilioni hadi kukamilika kwake na unatarajiwa kukamilika  septemba 22 ,2022 .

Aidha maabara hiyo ambayo ni ya pili kwa ukubwa Afrika  inatekelezwa na mkandarasi Li Jun Development Construction Company Ltd ambapo ujenzi huo umefikia asilimia 97 na kukamilika kwake kutaongeza tija  katika utekelezaji wa  sera  ya Taifa  ya Teknolojia  ya Nyuklia ya mwaka 2013.

Hayo yalisemwa jijini Arusha na Mkurugenzi mkuu wa Tume ya nguvu za atomu Tanzania ,Profesa Lazaro Busagala wakati kamati ya kudumu ya  bunge ya huduma na maendeleo ya jamii ilipotembelea  Tume hiyo kujionea maendeleo ya mradi huo.


Profesa Busagala alisema kuwa,uwepo wa  maabara hiyo  utasaidia kuzalisha wataalamu zaidi katika nyama ya teknolojia ya nyuklia ili kusaidia kukuza  uchumi  kupitia mchango wa  teknolojia ya nyuklia  katika sekta za afya,kilimo,mifugo,barabara  na maji. 

"Kupatikana kwa kituo cha mafunzo katika jengo la maabara hiyo  kutaongeza  wastani hadi kufikia  wataalamu 1000 kwa mwaka katika nyanja  mbalimbali na kuweza kuimarisha mfumo wa  usimamizi wa  usalama wa watu na mazingira imara uchimbaji  na usafirishaji  wa madini ya Urani  utakapoanza."alisema .

Profesa Busagala alisema kuwa,maabara  hiyo itasaidia sampuli mbalimbali za mazingira  na kusaidia kutoa elimu kwa umma ,kwani  kwa sasa maabara zilizopo  zinaweza kupima jumla ya sampuli  za mazingira  800 kwa mwaka na kuwepo kwa maabara hiyo kutasaidia  kupima sampuli 3000 za mazingira  ambapo matokeo yake yatasaidia kuongeza taarifa za kiusalama za mionzi. 

Naye Mwenyekiti wa  kamati hiyo Stanslaus Nyongo ambaye pia ni  Mbunge wa Maswa Mashariki  kuwa, wameridhishwa na ujenzi wa maabara  hiyo ambayo imeonyesha uhalisia wa thamani ya fedha zilizotumika huku akipongeza mradi huo kukamilika kwa wakati .

Nyongo alisema kuwa,wamekuwa wakihamasisha na kusimamia  matumizi salama ya mionzi katika kuhakikisha watanzania  hawaathiriki na mionzi hiyo kwa namna yoyote ile  ,hivyo uwepo wa  maabara hiyo ni  fursa kubwa sana kwani ni  maabara ya pili kwa ukubwa Afrika.

"Sisi kama kamati tumeridhishwa na utekelezaji wa mradi huu  na tunamwomba katibu mkuu wa  wizara  kuendelea kumsisitiza mkandarasi kukabithi  mradi  huo kwa wakati kulingana na tarehe iliyopangwa ili kutoa fursa kwa shughuli mbalimbali kuweza kuanza rasmi katika maabara hiyo."alisema Nyongo.










Share To:

Post A Comment: