MKUU wa mkoa wa Arusha, John Mongella amezindua mradi wa uhifadhi wa mazingira kwa kutumia maarifa ya asili ambao utatekelezwa na shirika la wanahabari la usaidizi wa jamii za Pembezoni (MAIPAC) na Shirika la CILAO unafadhiliwa na shirika la msaada la umoja wa mataifa (UNDP),Mfuko wa mazingira duniani na mashirika mengine ya kimataifa.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mongella amepongeza shirika la kimataifa la UNDP kwa ushirikiano na mashirika mengine, kuamua kutoa ufadhili MAIPAC na CILAO, ili waweze kuendesha mradi huu ambao unatarajiwa kusaidia suala zima la utunzwaji wa mazingira nchini kwa kutumia maarifa ya asili.

“Nimeelezwa mradi huu, unalenga kukusanya taarifa njia za video na maandishi za maarifa ya asili katika uhifadhi wa mazingira, utunzaji wa vyanzo vya maji,misitu na mabadiliko ya tabia nchi, lakini pia kutoa elimu ya uhifadhi wa mazingira katika wilaya hizi tatu” amesema.

Akisoma hutuba hiyo ya Mongella, Afisa Maendeleo ya jamii mkoa wa Arusha, Blandina Mkini amesema mradi huo umekuja wakati muafaka kwani sasa dunia inapita katika kipindi kigumu cha athari za mabadiliko ya tabia nchi, ambazo zinatokana na uharibifu wa mazingira na matumizi makubwa ya nishati ambazo sio rafiki kwa mazingira.

“Kwa mara ya kwanza, naona mradi kama huu,utatekelezwa na wanahabari, hili ni jambo jema kwani watasaidia sana kuelimisha jamii juu yetu kwa sababu wao ndio wamekuwa wakifanya jukumu hilo la kupasha habari” amesema.

Amesema mradi huo, utakwenda kusaidia watungaji wa sera na wadau wengine, kuingiza maarifa ya asili katika mikakati ya kutunza mazingira badala ya kuamini jamii hazina ujuzi wa asili wa kuhifadhi wa mazingira.

Kwa upande wake, Mkini amesema ofisi ya msajili msaidizi wamashirika yasiyo ya kiserikali mkoa Arusha, inapongeza kazi nzuri za MAIPAC na ipo tayari kutoa ushirikiano zaidi kuhakikisha mradi huo unafanikiwa.

Mratibu wa miradi midogo wa shirika la UNDP, Faustine Ninga amesema UNDP imetoa ufadhili katika mradi huo kwa kudhamini umuhimu wa maarifa ya asili katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi.

“Sio kwamba hatuamini elimu ya kisayansi lakini tunataka elimu hizi mbili zifanye kazi pamoja kwa ufasaha zaidi, kwani kuna nchi zinafanya vizuri sana katika matumizi ya elimu ya asili katika uhifadhi wa mazingira” amesema.

Amesema mradi huu utasaidia kurithisha maarifa ya asili kutoka kizazi kimoja hadi kingine baada ya kukusanya simulizi za wazee katika uhifadhi wa mazingira na kuziweka katika mfumo rasmi.

“Tunaimani MAIPAC itatekeleza vizuri mradi huu ili kuvutia wadau wengine ambao wanataka kuendeleza miradi ya mazingira kwa jamii za pembezoni” amesema.

Mkurugenzi wa MAIPAC, Mussa Juma amesema mradi huo utakuwa na manufaa makubwa na unatarajia kushirikisha makundi ya wanawake, vijana na wazee katika wilaya hizo la Longido, Monduli na Ngorongoro.

Juma amesema kwa kiasi kikubwa mradi huu utashirikisha vyombo vya habari katika kukusanya taarifa na kutoa elimu juu ya maarifa ya asili ya masuala ya uhifadhi wa maziungira katika jamii za pembezoni.

Wakizungumza katika Uzinduzi huo, Afisa Misitu na mazingira wilaya ya Monduli ,Habibu Mwanga, Afisa maendeleo ya jamii wilaya ya Longido,Grace Mgase na David Magembe Afisa Misitu wilaya ya Ngorongoro, walieleza mradi huo utakuwa na umuhimu mkubwa katika jamii na kuahidi kushirikiana na MAIPAC na CILAO.

Mwanga amesema kwa wilaya ya Monduli, Mradi utatekelezwa Kata za Selela na Engaruka, huku Magembe ameeleza mradi kutekelezwa msitu wa Engusero sambu na Ngese ni katika maeneo vijiji vya Olbomba na Kimotowa

Mkurugenzi wa CILAO, Odero Odero amesema katika mradi huo, wanatarajia kwa jamii na watunga sera watakuwa na uelewa mpana juu ya maarifa ya asili.


Share To:

Post A Comment: