Na Ahmed Mahmoud

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Nchini (TFF)  Wallace Karia amefanya mkutano na Uongozi wa Mkoa wa Arusha juu ya  maandalizi ya kufanyika kwa mkutano mkuu  wa shirikisho la mpira wa miguu Barani Afrika CAF.

Mkutano huo utafanyika hapa nchini mapema ifikapo mwezi wa nane tarehe 10 Mkoani Arusha, huku viongozi wa mashirikisho ya mpira wa miguu Afrika wakitajwa kuhudhuria Mkutano huo, wachezaji wa zamani  wa mpira wa miguu Afrika pamoja na Rais wa Shirikisho la mpira wa miguu Duniani (FIFA) Gianni Infantino

Kupitia mkutano huo Rais Karia amesema watatumia Fursa hiyo kufanya utalii wa kimichezo pamoja na utalii wa kimikutano lengo likiwa kuunga mkono juhudi za Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan za kutangaza utalii wa ndani huku Serikali ya Mkoa wa Arusha ikiwa katika hali nzuri ya maandalizi hayo.

Rais wa TFF Walace Karia amesema mkutano wa CAF utasaidia kukuza sekta ya Utalii nchini sanjari na mpira wa miguu nchini ikiwa ni kujipanga kwa wageni hao kufikia sehemu nzuri.

Amesema kwamba maandalizi ndio yameaanza kuelekea mkutano huo wa shirikisho la mpira barani Afrika utakaofanyika nchini mkoani Arusha mwezi wa nane Mwaka huu.

"Tutumie mpira kukuza sekta ya utalii nchini Leo tumekuja kuandaa sehemu watakazofikia wageni wetu kuelekea mkutano wa CAF utakaofanyika hapa nchini mwezi wa nane" Alisema Karia.

Kwa Upande wake Mkuu wa Mkoa wa Arusha John Mongela amesema wananchi wa mkoa huo wajipange sawa sawa na fursa ya mkutano huo ili kuendeleza maendeleo ya michezo na kiuchumi kwa mkoa wetu.

Amebainisha kwamba mkutano huo utaenda kuleta chachu ya maendeleo kama mkoa tutajipanga kisawa sawa kufanikisha mkutano huo mkubwa ambao umekuja Wakati wa msimu mkubwa wa Utalii nchini. 

"Tumejipanga kama mkoa kupokea mkutano huo kwani utafanyika Wakati muafaka kuelekea msimu wa Utalii kwa ukanda huu hivyo niwaombe wanaarusha tuungane pamoja kuhakikisha tunafanikisha mkutano huo ili kukuza sekta ya utalii na kipato kama mkoa" 






Share To:

Arusha Newsroom

Post A Comment: