Julieth Ngarabali,   Kibaha. 


Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge ametoa wito kwa wafanyabiashara wote wa vyakula wafanye wepesi kwa wanaofunga wasiongeze bei ya vyakula kwa sababu huu sio mwezi wa kuchuma faida kwa kuongeza bei kwenye Futari.


Mkuu wa Mkoa wa Pwani amewataka wafanyabiashara hao wachume dhawabu kwa kuwafanyia hisani ,vyakuka vipatikane na ikiwezekana kwa bei nzuri tuu kila mmoja amudu kupata futari na itasaidia kuleta umoja na upendo.


Ametoa wito huo Aprili 20 akizungumza na waumini wa Masikti wa Masjid E Maria  mara baada ya kushiriki Ibada ya pamoja ya  Adhuhuri  na kufungua msikiti huo huko Visiga kwa Kipofu mjini Kibaha sambamba na kugawa sadaka ya Futari iliyotolewa na taasisi ya  Miraaj  Tanzania Islamic Centre.


"niwaombe sana kutambua umuhimu wa mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani ni kipindi cha Ibada watu wanafunga wanahitaji futari hivyo niwaombe sana tuwafanyie wepesi wanaofunga tusiongeze bei bila sababu Serikali inautaratibu wa namna bei inavyotakiwa vinginevyo kwanza hatuwatendi wema,pili tunakiuka maadili yetu kama wa Tanzania,upendo ,kuheshimiana na tatu tunakiuka taratibu za ki Serikali"amesema.


Kunenge ameishukuru taasisi ya Miraaj  Tanzania Islamic Centre kutoa sadaka hiyo ya Futari kwani ni jambo jema na hasa wakati huu wa Mfungo wa Ramadhani 


Ameongeza kuwa Serikali haina Dini lakini wananchi wana dini zao mbalimbali , na Serikali inatoa haki ya watu wake kuabudu na tunaamini kabisa kwamba wananchi ambao ni wacha Mungu kwa imani zao basi wanasaidia nchi kuwa na amani ,utulivu na inapata baraka kutokana na sala na maombi yao.


Awali Mwenyekiti wa Taasisi ya Miraaj Tanzania Islamic Centre  Arif Surya amesema wametoa futari ya vyakula ikiwemo sukari, ngano, sembe, mchele, maharage na mafuta ya kupikia kwa waumini zaidi ya 200  na pia wamewajengea Msikiti huo ili kuwapa fursa ya kufanya ibada .


Surya pia ameomba taasisi zingine kushirikiana katika kazi nzuri kama hiyo ya kutoa misaada kwa jamii kupitia Ofisi ya Mufti wa Tanzania kwa sababu Mheshimiwa Mufti wa Tanzania anahimiza umoja na ushirikiano .


Baadhi ya Waumini walioswali msikitini hapo na kupata sadaka hizo akiwemo Hussein Shomari  na  Amina Gungu wameshukuru kupelekewa futari na kujengewa Msikiti huo kwa sababu awali walikua wakifata huduma za ibada mbali .

Mwisho.




Share To:

JUSLINE

Post A Comment: