Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu Mhe. Prof. Joyce Ndalichako amewataka Viongozi na Watumishi katika ofisi hiyo kuzingatia weledi, nidhamu na maadili ya utumishi wa umma ili waweze kutoa huduma bora kwa wananchi.

 

Waziri Ndalichako ameyasema hayo Machi 22, 2022 katika Ukumbi wa Mkutano uliopo jengo la Wakala wa Usalama Mahala pa Kazi (OSHA), Jijini Dodoma wakati akifungua Baraza la Wafanyakazi la Ofisi hiyo na kupokea pamoja na kujadili taarifa ya utekelezaji wa bajeti ya Wizara hiyo na makadirio ya bajeti mwaka 2022/2023 ambapo alihimiza viongozi na watumishi kufanya kazi kwa kufuata misingi na maadili ya utumishi wa umma katika kuhudumia wananchi kama ilivyokusudiwa na Serikali. 

 

Alieleza kuwa, wajibu wa kila mtumishi kufanya kazi kwa bidii na nidhamu ya hali ya juu huku akisisitiza uwepo wa mabaraza ya wafanyakazi katika maeneo ya kazi ambayo yamekuwa ni chachu ya kuongeza ufanisi na tija kwa wafanyakazi kwa kusaidia kuimarisha ushirikiano baina ya wafanyakazi na waajiri ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa weledi.  

 

“Serikali imeonyesha juhudi kubwa za kuhakikisha watumishi wote wa Umma wanafanya kazi kwa weledi na nidhamu kwa lengo la kufikisha huduma bora kwa wananchi wote,” alisema 

 

“Ni matumaini yangu kwamba kupitia mabaraza haya ya wafanyakazi tutaweza kuimarisha mshikamano, kufanya kazi kwa umoja, hivyo tuhakikishe ushauri na mawazo yatakayotolewa na watumishi katika mabaraza itakuwa ni chachu ya kuhamasisha tija katika utekelezaji wa majukumu yetu sambamba na kuzingatia Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo, alisema Ndalichako 

 

Ameongeza kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu imepata mafanikio makubwa katika kipindi cha mwaka moja wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo shughuli mbalimbali katika sekta hiyo zimefanyiwa kazi kwa wakati.

 

“Tuendelee kuhakikisha maelekezo yote yanayotolewa na Mheshimiwa Rais katika kukuza uchumi wa Taifa letu ili uwafikie wananchi kikamilifu yanafanyiwa kazi kwa ufanisi na wakati,” alisisitiza Prof. Ndalichako 

 

Hali kadhalika, Waziri Ndalichako amewataka viongozi wa TUGHE kuendelea kushirikiana na Uongozi wa ofisi hiyo pamoja na watumishi. Pia aliwasihi watumishi kujiepusha na vitendo vya rushwa.

 

Sambamba na hayo aliwahamasisha watumishi kuwa wabunifu na kushirikiana kwa pamoja ili kuendelea kuimarisha utendaji kazi wa majukumu yao.

 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la TUGHE tawi la Ofisi hiyo Bw. Godfrey Chacha alieleza kuwa Baraza pamoja na majukumu mengine lina kazi ya kupanga mipango na kushauri viongozi na watumishi kuhusu ufanisi wa kazi na hatua zinazotakiwa kuchukuliwa kuhakikisha kuwa huduma zinatolewa kwa wakati na kwa ubora unaokubalika ili kufanya kazi kwa uadilifu.

Share To:

Post A Comment: