Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula. Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Allan Kijazi (wa pili kushoto) akipata maelezo kuhusiana na mradi wa ujenzi wa nyumba za Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) eneo la Chamwino kutoka kwa msimamizi wa ujenzi Grace Musita wakati alipotembelea miradi ya NHC ya Iyumbu na Chamwino jijini Dodoma. Kushoto ni Mkurugenzi wa NHC Dkt Maulid Banyani. Mkurugenzi wa Shirika la Nyumba la Taifa Dkt Maulid Banyani (Kulia) akifafanua jambo mbele ya Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Allan Kijazi wakati Katibu Mkuu alipotembelea mradi wa ujenzi wa nyumba za NHC Chamwino mkoani Dodoma tarehe 8 Machi 2022. Kushoto ni Msimamizi wa ujenzi huo Grace Musita.

***********************

Na Munir Shemweta, WANMM

Wakati Serikali ya Awamu ya Sita kitimiza mwaka mmoja Machi 19, 2022 Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula ameanika mafanikio ya serikali hiyo katika kipindi cha mwaka mmoja katika sekta yake na kueleza kuwa sekta hiyo imepiga hatua kubwa katika masuala mbalimbali ikiwemo usajili wa hati na kuongeza kasi ya upimaji ardhí nchini.

Aidha, Dkt Mabula amesema, Serikali ya Mhe. Samia pia imeiwezesha wizara yake kupitia miradi mbalimbali kuhakikisha inapanga, inapima na kumilikisha ardhí nchini.

Akizungumzia mafanikio ya serikali ya awamu ya sita kwa Wizara yake tarehe 8 Machi, 2021, Dkt Mabula alisema katika kipindi cha mwaka mmoja Wizara ya Ardhi imeweza kupatiwa shilingi Bilioni 50 kama mkopo kwa ajili ya Program ya Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi (KKK) katika mbalimbali halmashauri nchini.

Mbali na kiasi hicho, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mhe. Samia Suluhu Hassan pia imeiwezesha Wizara ya Ardhi kupatiwa kiasi cha shilingi Bilioni 345 na Benki ya Dunia kwa ajili ya kuboresha Milki za Ardhi nchini

‘’Kwanza niishukuru serikali ya awamu ya sita chini ya Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuipatia Wizara yangu Bilioni 50 kwa ule mradi wa KKK pamoja na Bilioni 345 kutoka benki ya dunia kwa ajili ya kuboresha milki za ardí, fedha hizi zitatusaidia sana kuboresha milki za ardhí hasa ikizingatiwa ni asilimia 25 tu ardí yote ya Tanzania ndiyo imepimwa’’ alisema Dkt Mabula.

Mafanikio mengine ni pamoja na kusajiliwa Hatimiliki 41,533 pamoja na Hati za Sehemu ya Jengo 161 sambamba na kusajiliwa Hatimiliki 3,735 za kielektroniki kupitia mfumo wa ILMIS

Aidha, Dkt Mabula alibainisha kuwa, katika kipindi cha mwaka mmoja Wizara yake iliweza kukamilisha kazi mbalimbali za uthamini ikiwemo uthamini wa mali za wananchi kwenye ujenzi wa barabara ya pete (Ring Road) Jijini Dodoma wenye thamani ya shilingi bilioni 12.76 na ule Kijiji cha Fella Wilayani Misungwi kupisha ujenzi wa kambi (camping site) ya Mkandarasi kwa ajili ya ujenzi wa reli ya kisasa SGR Lot V.



‘’ Pamoja na kazi kubwa iliyofanyika kwenye suala la utahmini, Wizara imekamilisha pia majedwali ya fidia ya mali za wananchi 1,525 katika mkuza wenye urefu wa kilomita 89 ambapo shilingi 3, 818, 123,062 zitalipwa kama fidia kwa waathirika’’. Alisema Dkt Mabula.



Aliongeza kwa kusema kuwa, Wizara yake pia iliweza kutatua migogoro ya ardhí 745 katika mikoa na halmashauri mbalimbali nchini kupitia program ya Funguka kwa Waziri huku ikifanikiwa kukusanya shilingi 119,501,946.6 kupitia kodi ya Pango la Ardhi.



Kuhusu upimaji ardhi, Waziri Dkt Mabula alisema, Wizara ya Ardhi ilifanikiwa Kupima na Kuidhinishwa viwanja 232,599 pamoja na mashamba 353 huku ikinunua ndege ndogo isiyo na rubani (drone) kwa ajili ya kupiga picha za anga zitakazowezesha uandaaji wa ramani za msingi. Pia Serikali ya awamu ya sita chini ya Samia Suluhu Hassan ilitoa shilingi bilioni 2.7 kwa ajili ya uimarishaji mpaka wa Tanzania na Kenya.



Katika kuhakikisha Wizara ya Ardhi inashughulikia kero za wananchi kwa haraka, Dkt Mabula alisema Wizara yake imeanzisha Kituo cha Mawasiliano kwa Wateja (Call Centre) Ofisi ya Makao Makuu ya Wizara Jijini Dodoma kwa lengo la kuondoa chanagamoto katika sekta ya ardhi.



Kwa mujibu wa Dkt Mabula, katika kipindi cha mwaka mmoja Wizara ya Ardhi ilifanikiwa kuandaliwa Mipango ya Matumizi ya Ardhi ya vijiji 51 vinavyopitiwa na Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) katika Halmashauri za Singida (8), Iramba (5), Muheza (12), Kilindi (8), Nzega (12) na Chemba (6).



Akigeukia upande wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya, alisema katika kuboresha utendaji kazi wa Mabaraza ya Ardhi, wajumbe 151 waliteuliwa sambamba na kuanzishwa Mabaraza mapya ya Mbarali na Nkasi na kufanya idadi ya Mabaraza kuwa 60.



‘’Pamoja na maboresho kwenye mabaraza ya ardhi lakini pia tumerekebisha Sheria ya Mahakama za Utatuzi wa Migogoro ya Ardhi Sura ya 216 ili kuwezesha Wenyeviti wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya kuwa na ajira za kudumu badala ya ajira za mikataba’’. Alisema Dkt Mabula



Kwa upande wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Dkt Mabula alisema, Serikali ya mama Samia imeliwezesha shirika hilo kupata fedha za kukamilisha miradi yake mbalimbali iliyosimama pamoja na ile ya kimkakati.



Aliitaja baadhi ya miradi hiyo kuwa, ni machinjio ya kisasa ya Vingunguti mradi uliogharimu bilioni 12.5 ambayo ina uwezo wa kuchinja ng’ombe 1,500 na mbuzi 1,000 kwa siku, Hospitali ya Rufaa ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere iliyopo Kwangwa, Manispaa ya Musoma inaogharimu shilingi bilioni 17.2 na Ujenzi wa Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini iliyojengwa Mtwara eneo la Mikindani na kugharimu shilingi bilioni 15.8.



Katika hatua nyingine katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Allan Kijazi amekutana na waandishi wa habari kwenye eneo la mradi wa ujenzi wa nyumba za Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Iyumbu sambamba na kutembelea mradi wa nyumba wa Chamwino jijini Dodoma.



Katika mkutano huo Dkt Kijazi alisema, Shirika la Nyumba limeandaa mikakati kuhakikisha linakwamua miradi yote ya shirika hilo iliyosimama ikiwemo ya Morocco Square na Kawe.



Alibainisha kuwa, katika kufanikisha suala hilo, serikali ya awamu ya sita chini ya Samia Suluhu Hassan imeliruhusu shirika hilo kukopa fedha kiasi cha shilingi Bilioni 173.9 kwa ajili ya kukamilisha miradi yake ikiwemo ya Morocco Square, Kawe pamoja na Plot 300 Regent.



Dkt Kijazi alilipongeza shirika la Nyumba la Taifa kwa kubuni miradi ya ujenzi kwa kutumia wataalamu wa ndani na kubainisha kuwa ubunifu huo umelifanya Shirika kuingia kwenye ushindani wa ndani na nje katika masuala ya ujenzi.

Share To:

emmanuel mbatilo

Post A Comment: