Waziri wa maji Jumaa Aweso amesema kuwa  serikali kupitia wizara hiyo imetenga bilioni 4 kwaajili ya kutatua tatizo la maji katika Jimbo la Karatu mkoani Arusha kutokana  kiwango Cha uzalishaji wa maji kuwa milioni 1.6 huku mahitaji yakiwa milioni tano.

Aweso ameyasema hayo wakati akiweka jiwe la msingi katika mradi wa uhifadhi wa chanzo cha maji chemichemi za Qangdend ,mito ya Mang'ola na Baray iliyopo tarafa ya Eyasi wilayani Karatu ambapo alisema kuwa Karatu inahitaji kisaidiwa kuondokana na changamoto hiyo kutokana na kuwa ni mji wa kiuchumi na  maendeleo licha ya kutegemewa  kiutalii.


Sambamba na hayo alisema kuwa watanzania wana  kazi ya kulinda na kutunza vyanzo vya maji kama mboni ya jicho kwani matumizi ya maji yanaongezeka kila kukicha , kutokana na ongezeko la watu ambapo mwaka 1961 tulikuwa milioni 10 lakini hivi sasa makadirio yanaonyesha kuna watanzania milioni 50 hadi 60.


“Kulikuwa na chemchem  nyingi  na vyanzo vingine ikiwemo mito ambayo leo hazipo na ni kwasababu ya uharibifu wa vyanzo vya maji na uharibifu wa mazingira hivyo tutunze kwani maji ni uhai na hakuna mbadala, ukikosa maji unakaribisha maradhi,” Alisema Aweso.

 Aidha aliwaagiza maafisa wa rasilimali maji kuwashirikisha wananchi katika suala zima la kutunza vyanzo vya maji kwani wao binafsi hawawezi kuona uharibifu wote unaofanywa lakini wakiwashirikishwa na kuwafanya kuwa sehemu ya kulinda,ni dhairi  malengo ya kuwa na vyanzo endelevu yatatimia.

“Washirikisheni mipango yetu katika kulinda vyanzo hivi kwani hatuwezi kuona shughuli za kibinadamu zinafanyika na kuharibu vyanzo hivi, ulinzi wa vyanzo hivi vinaanza na Mimi, ukiyatunza mazingira yatakutunza na wewe  na jamii nzima, na  tusichokijua ni kuwa mazingira yana tabia ya kulipa kisasa ukiyahari yatakuharibu, ukiyatunza yatakutunza,”Alisisitiza Aweso.

Akisoma taarifa ya utekelezaji wa mradi huo mkurugenzi wa rasilimali za maji kutoka wizara ya maji Dkt George Lugomela  alisema kuwa vyanzo hivyo vinategemewa na vijiji saba vyenye jumla ya wananchi 44091 ambapo umegharimu kiasi cha shilingi milioni 578 kwa kutumia force akaunti ,ambapo wameokoa zaidi ya milioni 400  endapo wangetumia mkandarasi wa nje wangetumia bilioni 1.

“Lengo kuu la kuhifadhi vyanzo hivi vya maji ni kuvilinda na kuviendeleza kwa vizazi vilivyopo na vizazi vijavyo kwa kudhibiti shughuli za kibinadamu zilizokuwa zilifanyika ndani ya vyanzo hivyo lakini pia tumetoa elimu kuhusu umuhimu wa kutunza vyanzo vya maji ili kuzuia shughuli za kibinadamu ikiwa ni pamoja na kuhamasisha upandaji wa miti rafiki kwa mazingira hasa ya matunda,”Alisema Dkt Lugomela.

Mbunge wa Jimbo la Karatu Daniel Awakii alisema kuwa bonde hilo wanaoishi wakulima ambao ni wakulima wa vitunguu ambao kwa asilimia 80 ndio wanaiwezesha wilaya ya Karatu kupiga hatua za kimaendeleo kutokana na mapato yanayotoka kwa hivyo anaishikuri serikali kwa kutekeleza mradi huo lakini pia iendelee kutatua na changamoto za maji katika  jimbo hilo ili kila mwananchi aweze kupata maji safi na salama.

Naye Maiko Slaa katibu wa jumuiya ya  watumia maji bonde la kati miradi hiyo imechangia kiasi kikubwa alisema kuwa  juhudi za utunzaji wa vyanzo vya maji kwani kabla hali ilikuwa mbaya ambapo kulikuwepo na migogoro mingi ya matumizi ya maji ikiwemo kilimo kufanyika ndani ya vyanzo vya maji na hali ya mazingira ya vyanzo na hali ya mazingira ya vyanzo imekuwa salama, endelevu  na uoto wa asili umerudi.

“Bila ya miradi hii hali ya vyanzo vya maji ingekuwa hatarini kutoweka kwani awali mchanga na mafuriko ilikuwa ikiingia kwenye vyanzo na kuziba chemichemi, mifugo walikuwa wakinyweshwa kwenye vyanzo na kuleta uharibifu pamoja na shughuli za kilimo kufanyika ndani ya vyanzo vya maji na hifadhi ya mto,” Alisema Slaa.

Afisa mtendaji mkuu wa bonde la kati Danford Samson  alisema kuwa  uhifadhi wa vyanzo hivyo itasaidia kuongeza upatikanaji wa maji kati tarafa hiyo na kuwafanya wakulima kuendeleza kilimo cha kitunguu ambapo wataweza kunufaika na kuongeza kipato chao.

 “Lakini pia  wananchi wengi watafikiwa na kupata huduma ya maji  kwani bwawa hili lilikuwa lilikuwa linapeleka mchanga katika chanzo cha maji na kwa kuzuia chanzo kitaenda kuimarika na kuwa endelevu,”Alisema.

Share To:

Post A Comment: