Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu akizungumza na Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa (MSD) Meja Jenerali Gabriel Mhidze Dk. (kushoto) wakati wa ziara yake ya siku moja ya kutembelea Bohari hiyo iliyopo Keko jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa (MSD) Meja Jenerali Gabriel Mhidze Dk. akiwa na Mfamasia Mkuu wa Serikali Daud Msafi wakati wa ziara hiyo.
Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu ameiagiza Menejimenti ya Bohari ya Dawa (MSD) kutatua changamoto za upatikanaji wa dawa katika vituo vya kutolea huduma za Afya nchini, kutoka asilimia 50 ya sasa hadi kufikia asilimia 90, ndani miezi mitatu.
Waziri Ummy ametoa agizo hilo leo alipotembelea Bohari ya Dawa (MSD) kuongea na menejimenti kuhusu changamoto za upatikanaji wa dawa nchini alizozipata kutoka baadhi ya vituo vya afya na wananchi.
Alisema lazima changamoto hii itatuliwe haraka iwekanavyo, huku akisisitiza upatikanaji wa dawa muhimu ambazo mwananchi anaandikiwa na daktari.
“Hakikisheni upatikanaji wa dawa muhimu zote Katika vituo vya kutolea huduma za afya Rais Samia Suluhu Hassan ametuwezesha kupata fedha za kununua dawa, hivyo hakuna sababu ya ukosefu wa dawa na hili nitalisimamia kikamilifu kuhakikisha dawa zinanunuliwa na kusambazwa kwenye vituo kwa wakati". alisema Waziri Ummy.
Aidha, Waziri huyo ametembelea maghala ya kuhifadhia dawa ya MSD, sambamba na kujionea vifaa mbalimbali vya maabara pamoja na vitendanishi vyake.
Kwa upande mwingine Waziri Ummy amempongeza Mkurugenzi wa MSD na timu yake kwa kufanya vizuri katika kusimamia uanzishaji wa viwanda vya ndani vya dawa na kuwataka kuendelea kubuni zaidi aina ya viwanda vitakavyozalisha bidhaa muhimu za afya ili kutatua changamoto za dawa na vifaa tiba nchini.
Mbali na hilo kiongozi huyo amefurahishwa na juhudi za MSD za kuwezesha upatikanaji wa mashine za kusafisha damu kwa bei nafuu ambazo zitapunguza gharama kwa zaidi ya asilimia 50.
Post A Comment: