WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka watanzania kushirikiana na kushikamana ili kuyapa thamani madini ya Tanzanite na kuifanya dunia nzima itambue kuwa madini ya Tanzanite yanapatikana Tanzania tu na tayari imeweka mazingira ya kuyaongezea thamani.

 

Mheshimiwa Majaliwa ameyasema hayo leo (Jumatano, Januari 26, 2022) alipozungumza na wananchi katika eneo la EPZA unapojengwa Mji wa Tanzanie katika Mji Mdogo wa Mirerani wilayani Simanjiro akiwa katika ziara ya kukagua miradi ya maendeleo mkoani Manyara.

 

Waziri Mkuu amesema Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan itahakikisha rasilimali zote zilizoko nchini yakiwemo madini ya Tanzanite zinawanufaisha wananchi wote hususani wanaoishi katika maeneo zinapopatikana. “Watanzania lazima tushirikiane na tushikamane kuyapa thamani madini hayo.”

 

Amesema kuwa Serikali itaendelea kukutana na wafanyabiashara wa sekta madini kwa lengo la kuhakikisha kwa pamoja wanaweka mikakati ya kusaidia kuikuza sekta hiyo ili iendelee kuleta tija kwa watanzania na taifa kwa ujumla.

 

Akizungumza baada ya kukagua eneo la uwekezaji la EPZA, Waziri Mkuu amewataka watanzania kujitokeza na kuwekeza katika eneo hilo “Watanzania tumieni fursa ya eneo hili kuwekeza mtakapa faida”

 

Mheshimiwa Majaliwa aliwasisitiza wananchi waendelee kufanya biashara hiyo ambayo ina manufaa makubwa kwao na Taifa kwa ujumla na kwamba Serikali ipo tayari kuwahudumia wakati wote. “Tumejipanga kuwahudumia iwe wakati wa jua au wakati wa mvua.”

 

Naye, Naibu Waziri Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi amemuahidi Waziri Mkuu kuwa watahakikisha wanasimamia ujenzi wa eneo hilo ili liweze kukamilika kwa wakati na kuanza kutoa huduma iliyokusudiwa kwa watanzania wenye nia ya kuwekeza.

Share To:

Post A Comment: