MKURUGENZI wa Kampuni ya Usafiri ya Tashirif Salum Said akizungumza na waandishi wa habari leo ofisini kwake

Sehemu ya Abiria waliokwama kusafiri 

 

ABIRIA waliokuwa wakisafiri kwenda katika mikoa mingine kutokea kituo kikuu cha mabasi kilichopo Kange Jijini Tanga, walilazimika kuondoka saa moja asubuhi badala ya saa kumi na mbili, baada ya kampuni ya mabasi ya Tashiriff kuyazuia katika lango kuu la kutokea. 

Kadhia hiyo ya abiria kuchelewa kuondoka ilitokea leo saa 12:00 asubuhi katika kituo cha mabasi cha Kange, baada ya basi la Tashiriff lenye namba za usajili T 369 DYD lililokuwa likitaka kutoka kwenda Masasi mkoani Mtwara kuzuiwa na maafisa wa LATRA wakidai basi hilo muda wake ni saa 12:30 na siyo muda huo wa saa 12:00 asubuhi. 

Baada ya kuzuiwa basi hilo halikuondoka katika lango kuu la kutokea licha ya kutakiwa kuondoka kupisha magari mengine yatoke lakini halikuondoka na badala yake Mkurugenzi wa kampuni hiyo aliyefahamika kwa jina la Salim Hamoud Said kuweka gari lake dogo kuzuia magari mengine. 

"Tajiri wa Tashiriff alifika na gari lake dogo pia alifunga geti, huku akilalamika kwamba LATRA inafanya upendeleo wa ratiba za kusafiri kwa mabasi mengine," alisema abiria mmoja aliyekuwa akisafiri kwenda Shinyanga na Kapricorn. 

Askari wa usalama barabarani waliokuwa katika kituo kikuu hicho cha mabasi, hawakufanya chochote licha ya abiria kulalamika kuchelewa kuondoka katika muda wa saa 12:00 asubuhi. 

Polisi wengine walifika na kumchukua mkurugenzi huyo wa Tashiriff saa moja asubuhi wakati ambao ndiyo mabasi karibu yote yaliyokuwa yakisafiri kwenda mikao mingine yaliondoka baada ya basi hilo kuondolewa muda huo. 

Akizungumza baadaye baada ya kutoka kituoni saa 13:00 mchana jana, alisema aliamua kufanya hicho kama njia mojawapo ya kufikisha kilio chake kwa serikali kuhusu hatua ya LATRA kushindwa kuwapa ratiba ya muda wa saa 12:00 asubuhi kwenda Mtwara. 

"Leo tumefanya mgomo kwasababu siyo haki tunayofanyiwa na LATRA, sisi basi letu linakwenda kilomita 950 halafu hawataki kutupa ratiba ya saa 12:00 kamili kama mabasi mengine kwanini?," alisema mmiliki huyo. 

Mmiliki huyo alisema mara kadhaa ameomba ratiba ya saa 12:00 amepewa lakini baada ya kuifanyia kazi wiki moja ananyang'anya karibu mara nne alishapewa na hajui ni sababu gani amekuwa anasumbuliwa. 

"LATRA wamenipa ratiba hii Januari 6 mwaka huu ya saa 12:00 leo wamenizuia nisiondoke muda huu wanataka niendelee na ratiba ya saa 12:30 na ndiyo maana tumeamua kugoma pale kituoni," alisema na kuitaka serikali ifuatilie kuona ratiba za mabasi Tanga kuna nini?. 

Hata hivyo, alisema basi yake ya kwenda Masasi mkoani Mtwara iliondoka saa 3:00 asubuhi hatua ambayo inasababisha abiria kuteseka njiani kwa kusafiri muda mrefu njiani. 

Kwa upande wa wamiliki wa mabasi mengine wakizungumzia kadhia hiyo walisema kwamba inatakiwa kukomeshwa na serikali kwasababu haiwezekani mmiliki mmoja anaamua kuzuia mabasi mengine halafu hachukuliwi hatua. 

Wakala wa kampuni ya mabasi ya Simba mtoto katika kituo hicho Saleh Issa alisema kwamba baada ya kampuni ya Tashiriff kufunga lango la kutokea walilazimika kutumia mlango wa kuingilia ili waweze kusafiri baada ya abiria wao kuanza kulalamika wakielezea sababu ya kwanini wametaka kuondoka muda huo wa asubuhi. 

Wakala huyo alisema walikuwa na abiria waliokuwa na tiketi za boti za kwenda Zanzibar  saa 12:00 mchana hivyo wanavyozidi kuchelewa nani atawalipa gharama za kukosa safari ambayo tayari waliiandaa. 

"Kiukweli tulilazimika kupita No entry tena ilikuwa saa 7:00 asubuhi maana mule ndani tulikuwa na abiria wanaokwenda Bandarini, uwanja wa ndege na wengine walikuwa na ahadi na madaktari wa Muhimbili," alisema Saleh na kuiomba serikali ilitazame suala hili ili lisijirudie tena. 

Kamanda wa polisi wa kikosi cha usalama barabarani mkoani Tanga Mrakibu wa Polisi (SP) Leopold Fungu alipoulizwa kuhusu suala hilo kwanza alisema linatakiwa kuzungumzwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Vyombo vya nchi kavu (LATRA) na si yeye. 

"Hilo tatizo la asubuhi na mabasi kuzuiwa nadhani watafute LATRA,  sisi tulimkamata mmiliki wa Tashiriff kisha tukamuachia tulimshitaki kwa kosa la Obstruction," alisema Kamanda Fungu. 

Akizungumzia suala hilo kwa njia ya simu, Meneja wa LATRA mkoani Tanga Kenedy Nyakabondo alipouliza sababu za kwanini wasiwape ratiba ya saa 12:00 kampuni hiyo ya Tashiriff, alisema atatoa majibu baada ya wiki tatu kwakuwa hayupo Tanga hivyo hadi arudi.

Share To:

TANGA RAHA BLOG

Post A Comment: