Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Mvomero Bi.Mary Kayowa akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo kwa wajasiriamali ambao ni wafugaji, wakusanyaji, wabebaji na wasindikaji wa maziwa na bidhaa za maziwa katika halmashauri ya wilaya ya Mvomero. Wajasiriamali ambao ni wafugaji, wakusanyaji, wabebaji na wasindikaji wa maziwa na bidhaa za maziwa katika halmashauri ya wilaya ya Mvomero wakifuatilia mafunzo yaliyoandaliwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) ili kuwajengea uwezo wa kuzalisha maziwa yaliyo bora na salama kwa afya.

****************************

NA MWANDISHI WETU

Wananchi wameshauriwa kuwekeza kwenye sekta ya maziwa kwa kuzalisha na kusindika maziwa yenye ubora na usalama ili kutoshereza mahitaji soko letu la ndani na hata nje ya nchi .

Wito huo umetolewa leo Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Mvomero Bi.Mary Kayowa katika ufunguzi wa mafunzo kwa wajasiriamali ambao ni wafugaji, wakusanyaji, wabebaji na wasindikaji wa maziwa na bidhaa za maziwa katika halmashauri ya wilaya ya Mvomero.Mafunzo hayo yameandaliwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS).

Amesema takwimu za mwaka 2019/2020 zinaonesha kuwa uzalishaji wa maziwa ya ng'ombe Tanzania ni lita bilioni 3.13 kwa mwaka, jumla ambapo kati ya hizo lita bilioni 3.11 zilizalishwa na wafugaji wadogo na lita milioni 17.8 kutoka mashamba makubwa.

"Kwa takwimu hizi inaonesha wazi kuwa wafugaji wadogo ni wengi kuliko wakubwa na ndio wanaopeleka malighafi kwa wingi katika viwanda vyetu". Amesema Bi.Mary.

Aidha Bi Mary amesema juhudi za makusudi zinahitajika kuhakikisha maziwa yanayotumika kwenye viwanda katika usindikaji, ubora wake unafahamika kabla ya kutumika.

Amesema tuelewe kwa pamoja kuwa uzalishaji wa maziwa mengi uende sambamba kukidhi viwango, ubora na usalama ili kulinda afya ya mlaji na kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

"Tukijibidiisha katika uzalishaji wa namna hiyo kutaifanya nchi yetu kujenga uchumi endelevu wenye nguvu, imara na wenye ushindani". Amesema

Pamoja na hayo amesema kupitia mafunzo hayo ni njia muafaka wa kuleta tija zaidi katika juhudi za kuliletea taifa maendeleo ya haraka kulingana na fursa zilizopo hasa kwenye sekta ya viwanda, ufugaji, biashara na maeneo mengine mengi.

Amesema kuwa kimsingi wajasiriamali wote nchini ikiwa ni pamoja na wasindikaji wanaojihusisha na maziwa na bidhaa zake wametambulika kuwa sehemu ya washiriki katika kukuza uchumi wa taifa kwasababu wanao mchango mkubwa katika kukuza pato la taifa na kutengeneza ajira kwa wananchi walio wengi.
Share To:

emmanuel mbatilo

Post A Comment: