Na. Angela Msimbira TAMISEMI
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali Mhe Ummy Mwalimu amesema walimu wanaotaka kuhama kutoka mijini kwenda vijijini ruksa, lakini wanaohamishwa kutoka vijijijini kwenda mjini tume ya utumishi wa walimu nchini ihakikishe kabla ya kuwahamisha wawe na walimu mbadala.
Akifungua mkutano wa baraza la wafanyakazi Tawi la Tume ya Utumishi wa Walimu leo Jijini Dodoma Waziri Ummy amesema kuwa ni marufuku kuhamisha walimu kutoka katika Halmashauri zilizoko pembezoni kabla ya kupeleka waalimu mbadala
Amesema kuwa uhamisho ni haki ya mtumishi lakini changamoto kubwa wengi wanataka kuhama kutoka Halmashauri za vijijini kwenda mijini, hili haliwezekani, lakini kama amekaa zaidia miaka mitatu na anahitaji kuhama ihakikishwe kunakuwepo na walimu mbadala wa kuziba nafasi inayoachwa na mwalimu anayehama.
Waziri Ummy amesema kuwa Serikali imejikita katika kutoa elimu bora kwa jamii kwa kuhakikisha kunakuwa na mazingira bora ya kufundisha na kujifunzia ni wajibu wa tume sasa kuhakikisha uwiano wa walimu unafanyika ili kutoa elimu sawa kwa watoto wote wa Kitanzania hasa katika Halmashauri zilizopo pembezoni.
Aidha ameitaka tume ya Utumishi wa Walimu kufanya tathmini ya kina kwa kuangalia uwiano wa waalimu kwenye shule za Msingi na Sekondari katika Mamlaka za Serikali za Mitaa lengo likiwa ni kuwa na takwimu sahihi za mahitaji halisi ya walimu na uwiano uliosawa katika Halmashauri.
Post A Comment: