Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa(CCM) wa Arusha Mhe. Zelothe Steven ameitaka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuharakisha kutoa msamaha wa kodi katika mashine za mizani ya Wilayani Longido, ili kuruhusu huduma za mizani kuanza mapema.

Ameelekeza hayo alipokuwa akikagua ujenzi wa mradi huo uliopo katika Barabara ya Longido na Namanga, mapema leo hii.

Aidha Mhe.Zelothe amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha zaidi ya  Bilioni 14 ili kituo hicho cha mizani kijengwe.

Amesema kukamilika kwa mizani hiyo kutarahisha shughuli mbalimbali ikiwemo ya mahusiano, biashara na usafirisha baina ya Tanzania na Kenya.

Nae, Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. John Mongella amesema mizani hiyo iliyopo Wilaya ya Longido itarahisisha shughuli zote  za kibiashara zifanyike kwa urahisi.

Amesema Serikali ya Mkoa wa Arusha kwa kushirikiana na TRA na TANROADS wataendelea kusimamia mradi huo kwa nguvu zote na kuhakikisha unaanza kufanya kazi kwa muda uliopangwa.

Mizani hiyo itasaidia sana kulinda Barabara ambazo Serikali imetoa fedha nyingi katika kuzitengeneza.

Mkuu wa Wilaya ya Longido Mhe. Nurdin Babu amesema, mizani hiyo itakuwa msaada mkubwa kwani itapunguza hadha za magari zinazotokea maeneno ya Longido na Namanga.

 Meneja wa Mradi wa Mizani injinia Samuel Mtawa Wakala amesema mradi huo ulianza Mei 2020 na ulitakiwa kukamilika Agosti 2021 na mpaka sasa umefika  88% ya utekelezaji.

Bwana Mtawa amesema wao kama Wakala wanaendelea kusimamia na kuhakikisha mradi unakamilika mapema na kuanza kazi na wanaendelea kufuatilia msamaha wa kodi ya mizani.

Mhe Zelothe Steven pamoja na Mhe John Mongella na Viongozi wengine wameendelea na ziara ya kukagua Miradi ya kimkakati katika Wilaya ya Longido ambapo walitembelea kiwanda cha Nyama cha Eliya Food Overseas, Soko la kuuza Mifugo na kituo cha forodha cha Namanga.


 





Share To:

TANGA RAHA BLOG

Post A Comment: