Na Mwandishi wetu, Simanjiro
MCHIMBAJI
maarufu wa madini ya Tanzanite Bilionea Saniniu Laizer, ameiomba
Serikali kufanikisha upatikanaji wa nishati ya umeme kwenye vijiji vya
jamii ya wafugaji Wilayani Simanjiro ili binadamu na mifugo ipate maji
yaliyochimbwa visimani.
Bilionea
Laizer amesema jamii ya wafugaji wa vijiji vya Lengasiti na
Olchoronyori wanatumia gharama kubwa kununua mafuta ya kusukuma maji ya
visima ili kunywesha mifugo yao.
Akizungumza
mbele ya Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro, Dk Suleimani Serera, mchimbaji
huyo maarufu amesema kuna visima vitatu vya maji eneo hilo ila hakuna
umeme wa kusukuma maji.
“Kati
ya visima vitatu vya maeneo hayo, kimoja kilichimbwa na serikali na
viwili nilichimba kwa gharama zangu ila hakuna nishati ya umeme hivyo
serikali itusaidie,” amesema Bilionea Laizer.
Amesema
gharama ya kununua mafuta ya diseli ya kuendesha mitambo hiyo ni kubwa
kwani lita 200 zinamalizika kwa siku mbili katika kuhudumia mifugo zaidi
ya 10,000.
Amesema jamii
ya wafugaji wa eneo hilo wanapaswa kuangaliwa na serikali kwa jicho la
huruma kwani umeme ukiwepo utarahisisha maendeleo yao.
Hata
hivyo, Dk Serera amesema Serikali itahakikisha eneo hilo linapatiwa
nishati ya umeme ili kufanikisha upatikanaji wa maji kwa urahisi hivyo
watu na mifugo kunufaika.
Dk
Serera amesema serikali itaunga mkono juhudi za wadau wa maendeleo
mfano wa Bilionea Laizer ambao wanatumia fedha zao kwa ajili ya
kunufaisha jamii inayowazunguka.
Amesema
meneja wa wakala wa usambazaji maji na usafi wa mazingira vijijini
(Ruwasa) wilaya ya Simanjiro mhandisi Joanes Martin ni kijana mchapakazi
atamuagiza afuatilie hilo.
"Miongoni
mwa vijana wachapakazi ninaowaamini hapa Simanjiro ni mkuu wa idara ya
maji yule mhandisi Joanes anachapa kazi vizuri atasimamia hili
lifanikiwe," amesema Dk Serera.
Amesema
serikali ilishahidi kuwa itahakikisha vijiji vyote vinapatiwa nishati
ya umeme hivyo na wao Simanjiro watahakikisha Rea inafika maeneo yasiyo
na umeme ili wapate maji.
“Tunafahamu
kuwa kuna umuhimu mkubwa kwa jamii hasa zilizopo pembezoni kupatiwa na
serikali huduma mbalimbali za maendeleo ikiwemo nishati ya umeme,”
amesema Dk Serera.
Post A Comment: