Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Dorothy Gwajima akizungumza na wandishi wa habari katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma wakati alipokutana na Viongozi wa Mkoa wa Dodoma na kusisitiza kuhamasisha wananchi kuchukua tahadhari ya Corona.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka akitoa maelekezo kwa Viongozi wa Mkoa wa Dodoma na Wilaya zake kuhusu kuchukua tahadhari za ugonjwa wa COVID-19.

 

Charles James,

SERIKALI imewataka viongozi ngazi ya Mikoa na Wilaya Nchini kuhakikisha kwamba wanahamasisha wananchi kuchukua tahadhari na hatua zote za kujikinga na ugonjwa wa COVID-19 'Corona'.

Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dodoma na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Dorothy Gwajima wakati alipokutana na viongozi wa Mkoa wa Dodoma na Jiji la Dodoma na kutembelea Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.

Waziri Gwajima pia amekiri kwamba katika wimbi la kwanza na la pili la ugonjwa wa Corona bidhaa za tiba asili zilisaidia katika mapambano dhidi ya ugonjwa huo huku akisisitiza kwamba hawajazifuta.

" Niwaombe viongozi wa mikoa yote nchi kuhamasisha na kutoa elimu kwa wananchi juu ya kuchukua tahadhari na hatua za kujikinga, maeneo yenye mikusanyiko kuwepo na watoa elimu.

Wananchi wavae barakoa, wawe na vitakasa mikono na kuwepo na maji tiririka kwenye maeneo yote yenye mkusanyiko, daladala pia watu wakae level siti na maeneo ya masokoni na makanisani kuwepo na maji tiririka na uvaaji barakoa," Amesema Waziri Gwajima.

Amesema watanzania tayari walishakutana na wimbi la kwanza na lile la pili hivyo wanapaswa kutumia uzoefu walioupata kwenye wimbi lililopita katika kuishi na wimbi la tatu kwa kufuata tahadhari zinazotolewa na wataalamu wa afya.

" Kama wimbi la kwanza na la pili tuliishi nalo basi hata hili la tatu tunaweza kuishi nalo kiuzoefu. Bidhaa za Tiba asili hatujazifuta na tunakiri hatutozifuta na hatutoziacha ni wazi zilitusaidia sana," Amesema Dk Gwajima.

Amesema kama ambavyo Rais Samia alisema ni kweli Tanzania tayari ina wagonjwa kadhaa wenye ugonjwa huo hivyo ni vema kila mmoja kuchukua tahadhari za kujilinda yeye na mwenzake.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka ametoa maagizo kwa Mkuu wa Kikosi cha Barabarani mkoani humo kuhakikisha maagizo ya daladala kupakia abiria level siti na ambaye atakaidi agizo hilo achukuliwe hatua.

RC Mtaka ameagiza pia mameneja wa masoko yote ya Mkoa wa Dodoma kuhakikisha maji tiririka yanakuepo kwenye masoko yao pamoja na kila mfanyabiashara kuvaa barakoa.

" Niwaombe wananchi wote kujilinda na kulinda wenzake, tukumbuke anakufa ni nafsi siyo Serikali hivyo tuchukue tahadhari, tuvae barakoa, tuepuke mikusanyiko isiyo na lazima na tunapotoka basi tubebe vitakasa mikono, tupunguze pia kugusana na kukumbatiana.

Kwenye maeneo ya biashara pia hatua zote za kujikinga zichukuliwe, na kwenye nyumba za ibada tuepuke kushikana mikono na vifaa vya kujikinga viwepo," Amesema RC Mtaka.

Share To:

Post A Comment: