Na Woinde Shizza 


Shule za msingi zipatazo 13 mkoani Arusha zimeingia makubaliano ya unywaji  maziwa shuleni kwa wanafunzi wake ili kujenga afya za watoto ikiwa ni mojawapo ya uboreshaji wa lishe kwa watoto.


Akisoma makubaliano hayo jana mwanasheria wa bodi ya maziwa nchini Edwin Bantukki alisema bodi hiyo ndio inasimamia mkataba huo na kila pakti moja ya maziwa itakayouzwa kiasi cha shilingi 10 fedha taslimu kitaingia katika bodi hiyo.


" Maziwa yatakayouzwa shuleni  ni yale yaliyosindikwa kwa ubora na siyo mengine na  endapo makubaliano hayo yatakiukwa na shule husika watatakiwa kuilipa kampuni gharama zote kutokana na kuvunja makubaliano hayo " alisema Bantukki.



Kaimu msajili bodi ya maziwa Tanzania Noely Byamungu alisema mpango wa watoto kunywa maziwa shuleni unatekelezwa kwa asilimia kubwa duniani ambapo alisema zaidi ya watoto mil. 100 wanakunywa maziwa na nchi 39 zinaripoti mpango huo isipokuwa nchi ya Tanzania.


"Sisi kama Tanzania hatupo kwenye mpango huu hivyo ndio tumeanza kwa mkoa wa Arusha kama mfano na nchi nzima itatekeleza mpango huu , na hii ni ili kuhimiza unywaji wa maziwa nchini " alisema Byamungu.


Mkurugenzi wa Kampuni ya chakula ya Galaxy  Irfhan Virjee  alisema mpango huo utaongeza idadi ya wanywaji maziwa na kupanua wigo wa biashara katika kampuni hiyo ambapo alisema wanazalisha lita 72000 kwa siku tofauti na awali wqlipokuwa wakizalisha lita 3000 kwa siku.


 Kwa upande wa Kaimu katibu tawala mkoa wa Arusha David Lyamongi aliwataka wakurugenzi wa halmashauri zote za Mkoa kuhimiza unywaji wa maziwa  shuleni pamoja na kujiunga katika mpango huo ulioanzishwa Jana lengo likiwa kuboresha lishe kwa watoto.


Shule zilizosaini mkataba huo ni pamoja na Shule ya msingi Leganga,Longido, Meru pamoja na Shalom huku shule  tisa zilizobaki zikitarajiwa kuweka saini ya makubaliano hayo hivi karibuni.



Share To:

msumbanews

Post A Comment: